Majimbo kumi na sita yafungua mashitaka dhidi ya utawala wa Trump
Muungano wa Majimbo kumi na sita nchini Marekani unaongozwa na California umefungua mashitaka dhidi ya utawala wa Donald Trump.
Imechapishwa:
Jumatatu wiki hii, mjini San Francisco, Jimbo la California lilifungua kesi dhidi ya uamuzi wa rais Donald Trump kutangaza hali ya hatari kwa taifa ili aweze kupata fedha za kujenga ukuta kupambana na wahamiaji kwenye mpaka wa Mexico.
Tangazo hilo "ni aibu kwa taifa," Gavana wa California ameandika kwenye ukurasa wake wa Twitter.
Kesi ya kwanza iliwasilishwa mara moja siku ya Ijumaa. Kundi la kutetea haki, Public Citizen, liliwasilisha kesi kwa niaba ya hifadhi asili, na wamiliki watatu wa ardhi katika jimbo la Texas ambao wamearifiwa huenda ukuta huo ukajengwa kwenye ardhi yao.
Mkuu wa sheria katika jimbo hilo la California Xavier Becerra amesema wanamfungulia mashitaka Trump mahakamani "kuzuia matumizi mabaya ya mamlaka yake".
Hivi karibuni rais Donald Trump alisema kuwa hana haja ya kutangaza hali ya dharura lakini alifanya hivyo kutokana na matumaini ya kupata fedha kwa haraka zaidi, lakini wachambuzi wanasema kauli hii huenda ikamtia mashakani katika kujitetea kisheria.
Baada ya siku 35 za kukwama kwa shughuli za serikali nchini Marekani na kushindwa kwa vita vya kwanza vya kisiasa, mpango huu wa hali ya dharura unamuwezesha Donald Trump kutopingwa na bunge la Congress ili kupata dola Bilioni 7 katika bajeti ya Pentagon lakini pia katika fedha za misaada kwa majanga ya asili na kupambana na madawa ya kulevya, ili kujenga ukuta wake dhidi ya wahamiaji.
Wabunge kutoka chama cha Democratic ambao ndio wengi bungeni wameahidi kuwa watazuia mpango huo wa Donadl Trump.