Trump asema uamuazi wa kuishambulia Syria kufikiwa hivi karibuni
Rais wa Marekani Donald Trump amesema uamuzi kuhusu hatua ya kuchukua nchini Syria, utafanywa hivi karibuni.
Imechapishwa:
Trump amesema anakutana na maafisa wake kuona hatua ya kuchukua baada ya madai kuwa, Syria ilitumia silaha za kemikali kuwashambulia raia katika mji wa Douma.
Naye rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema ni wazi kuwa silaha za kemikali zilitumika kuwashambulia raia wa Syria na kusisitiza kuwa inaunnga mkono mashambulizi dhidi ya wanajeshi wa rais Bashar Al Assad.
Marekani imekuwa ikifikiria kuishambulia Syria, hatua ambayo serikali ya Uingereza imesema pia inaunga mkono.
Watalaam wa kuchunguza iwapo silaha za kemikali zilitumiwa, wapo njiani kwenda nchini Syria kuchunguza madai hayo siku ya Jumamosi.
Syria imekuwa ikikanusha madai hayo huku Urusi ikisema, Mataifa ya Magharibi yanatumia njia hii kujaribu kutafuta njia ya kuishambulia Syria.
Moscow ambayo imeendelea kuisaidia Damascus kijeshi imeonya kuwa itatumia uwezo wake wa kijeshi kuzuia mashambulizi yoyote dhidi ya mshirika wake.