Papa Francis azuru Chile na Peru
Kiongozi wa Kanisa Katoliki Papa Francis ameanza ziara yake nchini Chile lakini kuna wasiwasi wa kutokea shambulizi. Awali kabla ya kuanza kwa ziara hiyo, kulitokea mahambulizi dhidi ya makanisa kadhaa.
Imechapishwa:
Tayari Papa Francis amewasili jijini Santiago na kukutana na maandamano kutoka kwa waumini wa Kanisa hilo ambao wanalalamikia ongezeko la madai ya unyanyasaji wa kimapenzi unaowahusisha makasisi wa Kanisa hilo.
Papa Francis amewasili nchini Chile ikiwa ni mwanzo wa ziara yake ya wiki moja nchini humo pamoja na nchi ya Peru. Sherehe za kumkaribisha Papa zimefanyika kwenye uwanja wa ndege wa Santiago.
Hii ni ziara yake ya kwanza nchini Chile tangu kuchaguliwa kwake,ziara hiyo ikikumbana na upinzani mkubwa kufuatia kashfa ya udhalilishaji wa kingono dhidi ya watoto unaodaiwa kufanywa na baadhi ya makaaisisi wa kanisa hilo nchini Chile.
Ziara hii ya Papa nchini Chile imetanguliwa na matukio ya kushambuliwa kwa mabomu makanisa matatu katika mji wa Santiago, mji mkuu wa Chile.
Tayari washambuliaji waliacha vipeperushi kwamba shambulio linalofuata litamlenga Papa. Rais wa Chile Michelle Bachelet amesema matukio yaliyotokea ncini mwake dhidi ya makanisha yalizua hali ya wasiwasi, lakini ameagiza vikosi vya usalama na ulinzi kuimarisha usalama.
Papa Francis leo anatarajiwa kukutana na waathirika wa ukatili wa kijeshi uliofanywa na dikteta Augusto Pinochet, ambapo pia zaidi ya nusu milion wanatarajiwa kuwa katika mkusanyiko katika maeneo ambayo Papa atayatembelea katika ziara yake.