Trump aendelea kuionya Korea Kaskazini
Vita vya maneno kati ya Marekani na Korea Kaskazini vinaendelea kushuhudiwa. Rais wa Marekani Donald Trump ameionya Korea Kaskazini kwamba itakiona cha mtima kuni iwapo itathubutu kukishambulia kisiwa cha Guam au eneo lolote la Marekani.
Imechapishwa:
Bw ametoa kauli hiyo saa chache baada ya Korea Kaskazini kutangaza kwamba ina mpango wa kurusha makombora manne karibu na kisiwa cha Marekani cha Guam.
“Korea Kaskazini itakumbwa na kimbunga cha ajabu ambacho ni mataifa machache yaliyowahi kukumbana nacho iwapo haibadili maamuzi yake, " amesema Donald Trump.
Akiongea Alhamisi Bedminster, New Jersey, Bw Trump alidokeza kuwa huenda taarifa zake kuhusu Korea Kaskazini hazijakuwa na ukali wa kutosha, licha ya kuionya Korea Kaskazini wiki hii kwamba itanyeshewa na "moto na ghadhabu" kutoka kwa Marekani.
Waziri wa Ulinzi wa Marekani James Mattis, amekazia kauli ya Donald trump akisema kwamba kwamba mzozo wa kivita na Korea Kaskazini utakuwa na madhara makubwa, huku akibaini kwamba juhudi za kidiplomasia kwa sasa zinaanza kuleta muafaka.
Hali ya wasiwasi imeanza kuongezeka wiki za hivi karibuni baada ya Korea Kaskazini kufanyia majaribio makombora mawili ya kuruka kutoka bara moja hadi nyingine mwezi Julai.
Umoja wa Mataifa hivi majuzi uliongeza vikwazo dhidi ya Pyongyang kutokana na mpango wake wa silaha za nyuklia.