Israel na Hamas watangaza kusitisha mapigano kwa masaa 12 hii leo
Jeshi la Israel na wapiganaji wa Hamas wamesema hii leo watasitisha mapigano kwa masaa 12 kuanzia saa 2 asubuhi wakati suala la kusitishwa kwa kudumu bado ni kitendawili kwa sasa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakielezea hatua hiyo Wapiganaji wa Hamas wamesema kundi lao na wapiganaji wengine huko Gaza wameafikiana na hoja ya kitaifa ya kujali ubinadamu,ambapo baadaye Israel nayo ilithibitisha kuwa itasitisha mapigano kwa kile ilichokiita ni kufungua dirisha la ubinaadamu katika ukanda wa Gaza.
Taarifa kutoka kwa wizara ya mambo ya ndani ya kundi la Hamas huko Gaza imetoa onyo kwa watu kutokaribia majengo yaliyolipuliwa na kambi za kijeshi kwa kuhofia masalia ya mabomu.
Hata hivyo kuliripotiwa ghasia mapema jumamosi na kuingiza mapigano hayo katika siku ya 19 ambapo mashambulizi ya anga ya Israel yameua takribani watu 19 wakiwemo watoto 4 wahudumu wa afya huko gaza wameeleza.
Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani John Kerry, Katibu Mkuu wa Umoja wa Matayfa Ban Ki Moon wamekuwa katika mstari wa mbele kupata mwafaka ambao hadi sasa haijabainika suluhu litapatikana lini.