DRC: TP Mazembe pia yajitolea kupambana dhidi ya Ebola
Timu ya soka ya Tout Puissant Mazembe, moja ya vilabu vikubwa vya bara la Afrika yenye makao yake mjini Lubumbashi, nchini DRC imejitolea kupambana dhidi ya ugonjwa hatari waa Ebola.
Imechapishwa:
Sherehe ya uzinduzi ilifanyika Alhamisi wiki hii mjini Lubumbashi wakati wa mchezo wa kirafiki kati ya Tout Puissant Mazembe dhidi ya Cercle Sportif Don Bosco, timu nyingine ya mpira wa miguuya mji huo.
Timu zote mbili zilikutana kwenye uwanja wa mpira wa Ferme Futuka, kilomita 30 kutoka katikati mwa mji wa Lubumbashi.
Wachezaji wa TP Mazembe walikuwa wamevalia jezi za rangi nyekundu na weupe, huku vijana wa Cercle Sportif Don Bosco wakivalia bluu na weupe. Lakini ujumbe ulikuwa mmoja kwenye jezi za timu zote mbili: "Ebola ishia hapo". "Ushauri ambao ninaweza kutoa kwa kaka zangu na dada zangu ni kuosha mikono yao kila mara baada ya kusabahiana kwa mikono na mmoja kati ya ndugu au marafiki," Sylvain Gohou, beki wa TP Mazembe, akiongeza kuwa ni vizuri kujizuia kusogelea au kugusa wanyama pori.
"Tunaomba ndugu zetu na dada zetu wote wajilinde! ", ameingeza Sylvain Gohou.
Mwanasiasa wa upinzani Moïse Katumbi, ambaye ni kiongozi wa TP Mazembe, amesema ana wasiwasi kuhusu idadi ya waathirika wa ugonjwa hatari wa Ebola. Watu elfu mbili waliofariki dunia kutoka na ugonjwa hatari wa Ebola, idadi hiyo ni kubwa sana, amesema. Pia ametoa wito kwa wananchi wa DRC kujitolea katika mapambano dhidi ya ugonjwa hatari wa Ebola. "Ikiwa kuna mtu atafariki kutokana na Ebola magharibi au mashariki, kaskazini au kusini, ni nchi hii ya DRC ndio itakuwa imepoteza. Tunapaswa kusema sote kwa pamoja Ebola 'ishia hapo' ! "
Lengo ni kwamba kila mechi itakayopigwa na TP Mazembe, iwe nchini au nje ya nchi, ujumbe huu utakuwa ukitolewa kwa raia: tuheshimu sheria za usafi ili kuzuia kuenea kwa virusi vya Ebola.
Kampeni ya "Ebola ishia hapo" ilianzishwa siku chache zilizopita na shirika la kiraia la LUCHA.