Pata taarifa kuu
UKIMWI-AFYA

Ukimwi na maambukizi yake kwa binadamu

Upungufu wa Kinga Mwilini (kwa kifupi UKIMWI; kifupisho cha Kiingereza AIDS) ni ugonjwa unaotokana na virusi ambavyo kwa Kiswahili vinaitwa kwa kifupi VVU ("Virusi vya UKIMWI"; kwa Kiingereza: HIV, yaani "Human Immunodeficiency Virus") na vinashambulia mwili kwa kuondoa nguvu zake za kupambana na maradhi.

Ukimwi unaua watu wengi duniani.
Ukimwi unaua watu wengi duniani. AFP
Matangazo ya kibiashara

Kwa mujibu wa daktari Beatrice Kamikazi wa hospitali Hippocrate, mjini Bujumbura, Burundi, UKIMWI ni ugonjwa hatari sana katika maisha ya binadamu kwa kuwa husababisha vifo (yaani kupotea kwa uhai wa watu hao). Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani, kufikia mwaka 2014 ugonjwa huu umeua watu milioni 39, hasa kati ya wanaoishi barani Afrika upande wa kusini kwa Sahara. Kwa mwaka 2015 pekee wamefariki watu milioni 1.2 na kati yao watoto wengi.

UKIMWI umekuwa na madhara makubwa katika jamii, kama ugonjwa wa mwili na kama chanzo cha ubaguzi. Kuna sintofahamu kuhusu UKIMWI kama vile kwamba, unaweza kusambazwa kwa kugusana tu bila ngono.

Ugonjwa huu pia unasababisha madhara ya kiuchumi ambayo ni makubwa, hasa kwa nchi maskini.

UKIMWI hadi hivi sasa haina chanjo wala tiba, lakini watu wanaweza kuuepuka ugonjwa huu kwa kuachana na ngono ambayo huweza kusababisha ugonjwa huo, pia wanaweza kujikinga nao kwa kuepuka kuchangia vifaa au vitu vyenye ncha kali.

Mfumo wa kingamwili na VVU

Kila mtu huwa na mfumo wa kingamwili ndani yake. Seli za ulinzi zinazunguka mwilini na kutafuta vidubini vya nje vinavyoweza kuleta mvurugo na zinaviharibu. Kati ya seli hizi za ulinzi ni seli nyeupe za damu (lukosaiti) ambazo ni muhimu sana, amesema Bi Kamikaze.

Ukimwi unasababishwa na VVU. Kama virusi vyote, VVU vinaingia katika mwili kwa kusudi la kuzaa. Virusi haviwezi kuzaa peke yake: vinahitaji seli vinapoweza kuingia ndani yake na kutumia mfumo wa seli kwa kunakili DNA yake.

Kwa kawaida virusi vinashambuliwa na mfumo wa kingamwili na kuharibika. Lakini VVU vina tabia mbili za pekee ambazo zinavifanya vvya hatari hasa:

vinafaulu mara nyingi kuepukana na seli za ulinzi mwilini

vinaingia hasa katika seli nyeupe za damu za aina "seli za T". VVU vikianza kuongezeka katika seli nyeupe ya damu vinadhoofisha na hatimaye kuharibu seli hii.

Maana yake VVU vinashambulia moja kwa moja seli ambazo ni sehemu ya kingamwili na zinazohusika kukinga mwili. Kuenea kwa VVU mwilini kunapunguza idadi ya seli za ulinzi na hivyo kupunguza kiwango cha kingamwili, kwa mujibu wa wataalam wa maswala ya afya.

Baada ya kupungua kwa kingamwili vidubini vingine vinaendelea kufika mwilini lakini sasa vinaenea zaidi kwa sababu seli za ulinzi zimekuwa chache. Kila ambukizo linaendelea kwa muda mrefu zaidi na hivyo mwili kwa jumla unateswa kwa muda mrefu zaidi.

Kadiri Ukimwi unavyoendelea vipindi vya magonjwa vinakuwa virefu zaidi na nguvu za mwili zinapunguapungua. Katika ngazi za mwisho idadi ya maambukizo inazidi uwezo wa mwili wa kupambana nayo na hapo mtu unakaribia kifo.

Dalili

UKIMWI ni ugonjwa wa mfumo wa kingamwili wa binadamu unaosababishwa na virusi vya ukosefu wa kinga mwilini. Mwanzoni, baada ya kuambukizwa, mtu anaweza kukumbwa na kipindi kifupi cha maradhi ya aina ya mafua. Kwa kawaida, hali hii hufuatwa na kipindi kirefu kisicho na dalili. Ugonjwa huu huendelea kutatiza kingamwili jinsi unavyozidi, hivyo kumfanya mtu kuwa katika hatari zaidi ya kupata maambukizi, ikiwa ni pamoja na maambukizi nyemelezi, na kansa ambayo kwa kawaida hayawaathiri watu walio na kingamwili njema.

Kuna awamu tatu kuu za maambukizi ya VVU: maambukizi makali, awamu fiche na UKIMWI.

Maambukizi makali

Kipindi cha kwanza kufuatia maambukizi ya VVU huitwa VVU vikali, VVU vya kimsingi au dalili kali za kudhibiti virusi. Watu wengi hupata maradhi ya mfano wa mafua au maambukizi ya mfano wa mononukleosi wiki 2 - 4 baada ya kuambukizwa ilhali wengine hawana dalili zozote kuu. Dalili hutokea katika asilimia 40-90 ya visa vyote na mara nyingi hujumuisha homa, tezi kubwa na chungu za limfu, inflamesheni ya koo, upele, maumivu ya kichwa, na/au vidonda vya kinywa na sehemu za uzazi. Upele huu, unaotokea katika asilimia 20 - 50 ya visa, hutokea katika kiwiliwili, na kwa kawaida huwa wa makiulopapula.

Baadhi ya watu pia hupata maambukizi nyemelezi katika awamu hii. Dalili za tumboni na utumboni kama vile kichefuchefu, kutapika au kuharisha zinaweza kutokea, sawa na dalili za kinuroni za niuropathia ya pembeni au sindromu ya Guillain-Barre.[7] Muda ya dalili hutofautiana, ingawa kwa kawaida huwa wiki 1 - 2.

Awamu fiche

Dalili za kwanza hufuatwa na awamu fiche (VVU visivyo na dalili au VVU vya muda mrefu). Bila ya matibabu, awamu hii ya pili ya historia asilia ya maambukizi ya VVU inaweza kudumu kutoka miaka 3 hadi zaidi ya miaka 20;[10] (wastani wa miaka 8).[11]Ingawa kwa kawaida mwanzoni kuna dalili chache, au hata zisiwemo, karibu mwishoni mwa awamu hii, watu wengi hupatwa na homa, kukonda, matatizo ya tumbo na utumbo, na maumivu ya misuli. Kati ya asilimia 50 na 70 ya wagonjwa pia hupata limfadenopathia ya mwili wote inayorejea, ambayo hudhihirika kwa uvimbe usio na kisababishi na usio chungu wa zaidi ya kikundi kimoja cha tezi za limfu (ila katika sehemu za uzazi) kwa zaidi ya miezi 3 hadi 6.

Ingawa watu wengi walioambukizwa VVU-1 wana kiwango cha virusi kinachoweza kutambulika, na ambacho bila matibabu kitaendelea na kuwa UKIMWI, idadi ndogo (5%) huwa na kiwango kikubwa cha seli za CD4+ (seli saidizi za T) bila matibabu ya kudhibiti virusi kwa zaidi ya miaka 5. Watu hao huainishwa kama wadhibiti wa VVU au watu wasioendeleza kwa muda mrefu, ilhali wale ambao pia hudumisha kiwango cha chini au kisichotambulika cha virusi bila matibabu hujulikana kama "wadhibiti hodari" au "wagandamizaji hodari", Daktari Kamikazi amebaini.

Ukosefu wa Kinga Mwilini

Ukosefu wa Kinga Mwilini (UKIMWI) hufasiliwa kwa msingi wa kiwango cha seli za CD4 + cha chini ya seli 200 kwa kila µL au kutokea kwa magonjwa maalumu yanayohusiana na maambukizi ya VVU. Bila matibabu maalum, takriban nusu ya watu walioambukizwa VVU hupata UKIMWI katika muda wa miaka 10. Hali zinazotokea mara nyingi zaidi kudhihirisha uwepo wa UKIMWI ni numonia ya numosistisi (40%), kakeksi kwa muundo wa dalili dhoofishi za VVU (20%) na kandidiasi ya umio. Dalili nyingine ni pamoja na maambukizi ya njia ya pumzi.

Maambukizi nyemelezi yanaweza kusababishwa na bakteria, virusi, kuvu na vimelea ambavyo kwa kawaida hudhibitiwa na mfumo wa kingamwili.Maambukizi yanayotokea hutegemea, kwa upande mmoja, aina ya viumbehai vinavyopatikana kwa wingi katika mazingira ya mtu.Maambukizi hayo yanaweza kudhuru karibu kila mfumo wa viungo.

Watu walio na UKIMWI wako katika hatari kuu zaidi ya kupata saratani nyingi zinazosababishwa na virusi, kama vile: Sakoma ya Kaposi, limfoma ya Burkitt, limfoma ya mfumo mkuu wa neva na saratani ya seviksi.[8]Sakoma ya Kaposi ndiyo saratani inayotokea mara nyingi, yaani katika asilimia 10 hadi 20 ya watu wenye VVU. Saratani inayoifuata ni limfoma, ambayo imesababisha vifo vya karibu 16% ya watu wanaoishi na UKIMWI, na ndiyo dalili ya kwanza ya UKIMWI katika asilimia 3 - 4 ya watu. Saratani hizi mbili huhusishwa na virusi vya hepesi ya binadamu aina ya 8. Saratani ya seviksi hutokea mara nyingi zaidi katika watu walio na UKIMWI kwa sababu ya jinsi inavyohusiana na virusi vya papiloma ya binadamu.

Isitoshe, watu hao mara nyingi huwa na dalili za kimfumo, kama vile homa ya muda mrefu, jasho (hasa usiku), tezi za limfu zilizofura, ubaridi, udhaifu na kupoteza uzito. Kuharisha ni dalili nyingine inayotokea katika takriban 90% ya watu wenye UKIMWI.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.