Togo: Maandamano ya upinzani yapigwa marufuku na mamlaka
Maandamano yaliyopangwa kupinga kuandikwa upya kwa Katiba mpya hayaruhusiwi. Kwa mujibu wa barua iliyotumwa na Waziri wa mambo ya Ndani kwa vyama kadhaa vya upinzani, Hodabale Awate anasema kuwa vyama hivi havikuheshimu muda wa notisi ya kisheria ya maandamano haya ya Aprili 11, 12 na 13 na kwamba, kwa sababu hiyo, maandamano hayo hayatofanyika.
Imechapishwa:
Wiki iliyopita vyama kadhaa vya upinzani vya Togo na mashirika ya kiraia viliitisha maandamano ya siku tatu siku ya Alhamisi kupinga kuahirishwa kwa uchaguzi wa wabunge na wa magavana, huku kukiwa na mvutano wa kisiasa unaoongezeka tangu kupitishwa kwa Katiba mpya mwezi Machi.
Vyama vinne vya upinzani (ADDI, ANC, FDR na PSR) na shirika la kiraia (FCTD) "vinatoa wito kwa watu kuungana nao kwa maandamano makubwa Aprili 11, 12 na 13", katika taarifa iliyotolewa kwa umma siku ya Alhamisi ya wiki iliyopita, na. "wanaomba wagombea kuendeleza kampeni nchi nzima".
Maandamano yamepigwa marufuku nchini Togo tangu mwaka 2022, baada ya shambulio kwenye soko kubwa la Lomé ambalo lilisababisha kifo cha askari mmoja. Wito huu wa kuandamana umekuja siku moja baada ya kutangazwa kuahirishwa kwa uchaguzi wa wabunge na wa magavana, ambao awali ulikuwa umepangwa kufanyika Aprili 20, ili, kwa mujibu wa mamlaka, kutoa muda kwa Bunge kuisoma kwa mara ya pili rasimu ya Katiba mpya ambayo iliidhinishwa Machi 25.
Baada ya sintofahamu iliyosababishwa na kupitishwa kwa Katiba hii mpya, ambayo inaihamisha Togo kutoka utawala wa rais hadi utawala wa bunge, Rais Faure Gnassingbé - madarakani tangu mwaka 2005 akimrithi baba yake ambaye tawala nchi hii kwa karibu miaka 38 - wiki iliyopita aliagiza wabunge kufanya tathmini ya rasimu ya katiba.