Ethiopia yawanyooshea kidole cha lawama waasi wa Tigray kwa kupuuzia mazungumzo
Serikali ya Ethiopia inawashtumu waasi wa Tigray kwa kutokuwa na utashi wa kushiriki kwenye mazungumzo ya amani ili kumaliza vita ambavyo vimekuwa vikiendelea kwa zaidi ya miezi 20 sasa.
Imechapishwa:
Serikali ya Waziri Mkuu Abiy Ahmed na waasi wa Tigray katika wiki za hivi karibuni, wamekuwa wakisema wako tayari kuzugumza lakini vikwazo bado vinashuhudiwa, wakati huu kila upande ukimlaumu mwenzake.
Msemaji wa Waziri Mkuu Abiy, Billene Seyoum amesema serikali imeendelea kutaka kufanyika kwa mazungumzo hayo, lakini waasi wa Tigray wanaonekana hawana nia ya amani.
Kumekuwa na mvutano kuhusu ni nani aongoze mazungumzo hayo, lakini pia waasi wa Tigray wanataka huduma zote zirejeshwe katika jimbo hilo kabloa ya kuanza kwa mazungumzo hayo.
Siku ya Jumatano, Kamati ya serikali iliyoteuliwa kuongoza mazungumzo hayo, ilitoa wito wa usitishwaji wa vita kama ilivyopendekezwa na Umoja wa Afrika.
Hayo yanajiri wakati Takriban nusu ya wakazi wa Tigray nchini Ethiopia wanakabiliwa na uhitaji mkubwa wa chakula huku mashirika ya misaada ya kiutu yakihangaika kufikia idadi kubwa ya watu kutokana na changamoto ya ukosefu wa nishati ya mafuta, kufuatia mzozo wa hivi karibuni uliodumu kwa miaka miwili.
Mnamo mwezi Machi serikali ya shirikisho ya Ethiopia ilitangaza kusitisha mapigano hatua iliotoa fursa kwa mashirika ya kiutu kutoa misaada.
Vita kati ya jeshi la Ethiopia na waasi wa Tigray, vilivyoanza mwezi Novemba mwaka 2020, vimewaacha mamilioni ya wakaazi wa jimbo la Tigray bila chakula, maji safi lakini pia wamekatiwa umeme.