Mjumbe wa Marekani kuzuru Ethiopia Alhamisi kutoa wito wa suluhu ya amani
Mjumbe wa Marekani katika Pembe ya Afrika Jeffrey Feltman atazuru Ethiopia siku ya Alhamisi Novemba 4 na Ijumaa Novemba 5 ili kutoa wito wa suluhu ya amani, huku mzozo ukiongezeka na makundi ya waasi yakiendelea kusonga mbele.
Imechapishwa:
"Marekani inazidi kuwa na wasiwasi kuhusu kuongezeka kwa mapigano na vurugu za kijamii, na inafuatilia hali hiyo kwa karibu," msemaji wa wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani amesema Jumatano, Novemba 3, 2021, akitangaza ziara hii ya Mjumbe wa Marekani katika Pembe ya Afrika Jeffrey Feltman.
Hayo yanajiri wakati Umoja wa Mataifa umetoa ripoti ukibaini kwamba mogoro wa Tigray unachochewa na 'ukatili uliokithiri'.
Pande zote katika mzozo wa Tigray zina hatia ya "uhalifu dhidi ya binadamu", inasema ripoti ya pamoja ya Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Kibinadamu na Tume ya Haki za Kibinadamu ya Ethiopia iliyowasilishwa Jumatano, Novemba 3.
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed amejibu haraka kuhusu ripoti hiyo. Amebaini kwamba ripoti hii inaondoa uwezekano kwamba mauaji ya halaiki yalifanywa huko Tigray. Kwa mujibu wa Abiy Ahmed ripoti hii inaonyesha "dhahiri kwamba tuhuma za mauaji ya halaiki ni za uongo na hazina ukweli wowote," amesema katika taarifa.