Serikali ya Ethiopia yatangaza kusitishwa kwa mapigano Tigray, TPFL likidai ushindi Mekelle
Serikali ya Ethiopia imetoa wito wa kusitishwa kwa mapigano katika jimbo lenye utata la Tigray, baada ya miezi nane ya mapigano kati ya wanajeshi wa serikali na wapiganaji wa TPLF waliotimuliwa kutoka eneo hilo, serikali ikisema hatua hiyo inalega kutoa nafasi kwa wakulima kufanya shughuli za upanzi.
Imechapishwa:
Haya yanajiri wakati huu wapiganaji TPLF, wakidai kuudhibiti tena mji mkuu wa Tigray, Mekelle, raia nao wakiripotiwa kusherekea hatua hiyo.
Serikali haijatoa taarifa kuhusiana na madai ya wapiganaji wa TPLF kuuchukuwa tena mji wa Mekelle.
Mapigano katika jimbo hilo yamechangia hali ya kibinadamu, umoja wa mataifa ukitoa wito mara kwa mara wa kusitishwa kwa mapigano .
Umoja wa mataifa unasema zaidi ya raia millioni tano wanahitaji chakula cha msaada jimboni Tigray, wengine 350, 000 wakikabiliwa na baa la njaa kipindi hiki.
Chama cha TPLF, kilikosa kuafikiana na serikali ya waziri mkuu Abiy Ahmed kutokana na sera yake ya mabadiliko ya kisiasa nchini Ethiopia, ila uvamizi wa TPLF kwa kambi ya jeshi eneo la Tigray ndio ulichangia serikali Abiy kuanza kuwakabili wapiganaji hao.
Pande zote katika mapigano hayo zimekashifiwa kwa mauwaji ya raia na kukiuka haki za binadamu.
Mataifa ya Uingereza, Marekani na Ireland, yameitsisha mkutano wa dharura na baraza la usalama la umoja wa mataifa kujadili hali katika jimbo hilo.