Kiongozi wa Tigray Debretsion Gebremichael afutilia mbali makataa ya kujisalimisha
Kiongozi wa Tigray Debretsion Gebremichael ameapa kuendelea na mapigano dhidi ya vikosi vya serikali kuu ya addis Ababa na kufutilia mbali makataa ya kujisalimisha yaliyotolewa hivi karibuni na Waziri Mkuu Abiy Ahmed.
Imechapishwa:
Siku ya Jumapili Waziri mkuu wa Ethiopia Abby Ahmed, alitangaza makataa ya saa sabini na mbili 72 kwa vikosi vinavyoongoza mapigano Kaskazini mwa eneo lenye utata la Tigray, kujisalimisha kwa serikali.
Debretsion Gebremichael amekanusha madai ya serikali kwamba mji mkuu wa eneo hilo Mekelle umezingirwa na vikosi vya serikali.
"Waziri mkuu haelewi sisi ni kina nani. Ni watu na misimamo yetu na tuko tayari kufariki dunia tukitetea haki ya kutawala eneo letu", Shirika la habari la AFP limemnukuu Bw. Debretsion, kiongozi wa chama cha Tigray People's Liberation Front (TPLF).
Chama cha TPLF kimekuwa kikitawala katika siasa za eneo hilo na kuna wakati kilikuwa kundi kubwa la waasi lenye nguvu na kuongoza mapigano ya kuondoa madarakani serikali iliyotangulia ya Ethiopia mwaka 1991.