Senegal: Macky Sall atangaza msaada wa CFA Bilioni 10 baada ya mafuriko
Rais wa Senegal Macky Sall ametangaza bajeti ya faranga za CFA bilioni 10 (zaidi ya euro milioni 15) kukabiliana na mafuriko yaliyoikumba nchi mwishoni mwa wiki iliyopita. raia na viongozi wa upinzani wamekosoa usimamizi wa mkasa huu unaotokea mara kwa mara katika kila msimu wa mvua.
Imechapishwa:
Baada ya mkutano wa dharura Jumanne na mawaziri wahusika, rais Macky Sall ameahidi hatua za dharura, kuendelea kwa mpango wa miaka kumi wa kupambana na mafuriko, na kuwataka raia wenzake "kubadili tabia".
"Tuko katika hali ya mabadiliko ya hali ya hewa, hali inayoikumba dunia kwa sasa", rais wa Senegal ameeleza. Mafuriko yaliyoikumba nchi mwishoni mwa wiki iliyopita yamegharimu maisha ya watu wasiopungua sita, kulingana na Wizara ya Mambo ya Ndani, na yamesababisha uharibifu mkubwa.
"Mapema mwaka 2012, nilizindua mpango wa miaka kumi wa kudhibiti mafuriko na ni muhimu mpango huu uendelezwe (...) Kwa hivyo kuunga mkono juhudi hizi, nimeamua kutenga bajeti ya Faranga za CFA bilioni 10, kati ya hizo bilioni 3 zitatumika moja kwa moja kusaidia watu walioathirika na bilioni nyingine 7 zitatumika kusaidia huduma za wazima moto, Onas (Ofisi ya Taifa ya Usafi wa Mazingira nchini Senegal) na ununuzi wa vifaa vya ziada, ”ameongeza rais wa Senegal.
Macky Sall ametangaza kwamba "hivi karibuni serikali itawasilisha hali ya mpango wa miaka kumi wa kudhibiti mafuriko na hasa mpango mpya wa ufadhili wa ziada kupatikana ili kukamilisha mpango huu wa miaka kumi".