Libya: Mji mkuu wa Tripoli wakabiliwa na hali ya sintofahamu
Makabiliano makali yametokea kati ya wanamgambo kufuatia kukamatwa kwa mamluki kadhaa kutoka Chad ambao ni sehemu ya "kundi la wahalifu" ambao "wamekuwa wanajihusisha visa vya wizi na uporaji", kulingana na mamlaka nchini Libya.
Imechapishwa:
Mamluki hao walikuwa chini ya uongozi wa Osama Jouili, mkuu wa vikosi vya majeshi Magharibi mwa Libya. Agizo la kuwakamata lililotolewa na Fathi Bachagha, Waziri wa Mambo ya Ndani wa serikali ya Umoja wa Kitaifa (GNA). Wawili hao ambao ni kutoka kambi moja ya kisiasa wako katika upinzani mkubwa.
Hii sio mara ya kwanza tofauti kati ya wanamgambo kutoka Magharibi mwa Libya kuzuka. Hii ilitokea mara kadhaa hapo awali, wakati na baada ya kushindwa kwa mashambulizi ya Mashal Khalifa Haftar ya kutaka kuuteka mji mkuu Tripoli.
Kulingana na ripoti kadhaa za Umoja wa Mataifa, wanamgambo nchini Libya sasa ni kama makundi, ambayo kila upande unatetea masilahi yake na kutafuta kunufaika kupitia mapato ya serikali wakati ukitumia udhaifu wake na ufisadi mkubwa uliokithiri.
Kulingana na wachunguzi, nia ya wanamgambo hao ni kutawala na kutoa ushawishi kwa kuchukuwa maamuzi ya kisiasa. Na, wakati masilahi ya wanamgambo hawa yanakinzana, hali huwa mbaya na mgawanyiko hujitokeza.
Lengo la msingi la Fathi Bachagha ni kuchukua udhibiti wa Tripoli kwa ushirikiano na wanamgambo kutoka Misrata. Hivi karibuni aliamuru kukamatwa kwa viongozi kadhaa wa wanamgambo huko Tripoli na wengine kufutwa katika miji kadhaa.