Uturuki yashtumu baadhi ya mataifa kuchochea vita nchini Libya
Uturuki imeshtumu mataifa yanayochangia mzozo nchini Libya, wakati huu ikijaribu kuisadia serikali ya Tripoli inayotambuliwa na umoja wa mataifa kuwa thabiti.
Imechapishwa:
Bazara la usalama wa taifa hilo linaloongozwa na rais Recep Tayyip Erdogan, limesema, Uturuki itaendelea kupigania haki za raia wa Libya dhidi ya vikosi vya Jenerali Khalif Haftar, ambaye anasaidiwa na nchi ya Urusi na kuungwa mkono na baadhi ya nchi za Kiarabu, ikiwa ni pamoja na Misri.
“Kuna wanaofanya juhudi ambazo hazitozaa matunda ili wafanikiwe katika mapigano nchini Libya, “ Uturuki imesema katika taarifa.
Hivi karibuni Misri ilitishia kuingilia kijeshi iwapo serikali ya GNA inayotambuliwa na jumuiya ya kimataifa, itaelekea kuuteka mji muhimu wa Sirte.
Wakati huo huo majeshi ya Serikali ya Tripoli kupitia msemaki wake, yaliapa kujibu mashambulizi yoyote kutoka nje ya mipaka ya nchi hiyo.
Libya imeendelea kukumbwa na machafuko tangu mapinduzi ya mwaka 2011 yaliyomuondoa madarakani rais wa nchi hiyo Muamar Ghadafi na sasa makundi hasimu ya kisiasa pamoja na makundi yaliyojihami wanapigania udhibiti wa nchi.