Uchaguzi wa urais Malawi: Rais Peter Mutharika apinga uamuzi wa mahakama
Rais wa Malawi Peter Mutharika anatarajiwa kukata rufaa uamuzi wa Mahakama ya Katiba kufutilia ushindi wake, baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Mei 2019.
Imechapishwa:
Kauli hii imetolewa na msemaji wake Mgeme Kalilani, hatua ambayo inaweza kusababisha machafuko zaidi nchini humo.
Majaji nchini humo baada ya kufuta uchaguzi huo na kubaini visa vya udanganyifu, waliagiza kuwa, uchaguzi mpya utafanyika baada ya siku 150.
Jaji kiongozi wa Mahakama ya Katiba, Healey Potani, amesema uchaguzi uliofanyika mwezi Mei ulikuwa na dosari nyingi zilizoufanya uchaguzi huo usiwe huru, haki na wa kuaminika.
Katika uchaguzi huo uliofanyika Mei 21 mwaka 2019, Tume ya uchaguzi (MEC) ilimtangaza Peter Mutharika kuwa mshindi wa uchaguzi kwa kupata asilimia 38.6 ya kura zote.
Matokeo hayo kwa majuma kadhaa yalisababisha maandamano makubwa ya wafuasi wa upinzani, huku serikali ikilaumiwa pakubwa kwa kutumia nguvu kubwa kukabiliana na waandamanaji.
Tume ya haki za binadamu nchini Malawi imesema mwezi Oktoba pekee wakati wa maandamano ya wafuasi wa upinzani, polisi na wanajeshi walitekeleza vitendo vya ukatili kwa kuwabaka wanawake hata mbele ya familia zao.
Licha ya upinzani kulalamikia matokeo ya uchaguzi huo, tume ya uchaguzi ilisisitiza kuwa ilifuata sheria katika kutangaza mshindi na kwamba hakukuwa na udanganyifu ambao ungefanya matokeo ya uchaguzi huo kuwa batili.