Umoja wa Mataifa kutuma mjumbe wake nchini Equatorial Guinea
Umoja wa Mataifa umesema utamtuma mjumbe wake nchini Equatorial Guinea baada ya serikali nchini humo kusema kuwa ilizuia jaribio la mapinduzi.
Imechapishwa:
Tayari UN imesema kuwa itamtuma Francois Lounceny Fall, mjumbe wake katika ukanda wa Afrika Magharibi wiki ijayo kushauriana na serikali ya Malabo.
Farhan Haq msemaji wa Umoja huo amesema kuwa, hakuna taarifa ya kutosha kuhusu madai ya kuwepo kwa mpango wa kumwondoa madarakani Teodoro Obiang Nguema, ambaye amekuwa madarakani kwa miaka 38 sasa.
Aidha, amesisitiza kuwa Umoja wa Mataifa unalaani mbinu zozote za kuchukua madaraka kwa nguvu.
Wizara ya Mambo ya ndani nchini humo imewashtumu wanasiasa wa upinzani kwa kuwatumia mamluki kutoka nchi za Chad, Sudan na Jamhuri ya Afrika ya Kati walioshambuliwa katika mpaka na Cameroon na maafisa wa usalama wa Equatorial Guinea.
Mwaka 2004, jaribio kama hili halikufanikiwa dhidi ya rais Nguema.