Polisi wavamia Kanisa Katoliki na kuwasambaratisha wauamini jijini Kinshasa
Maafisa wa usalama wamerusha mabomu ya kutoa machozi na kufwatua risasi hewani kusambaratisha waumini wa Kanis Katoliki waliokuwa wanaendelea na ibada jijini Kinshasa siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Waumini wa Kanisa Katoliki katika Manispaa ya Bandalungwa walikuwa wamepanga kuandamana kwa amani kushinikiza kujiuzulu kwa rais Joseph Kabila na kumtaka kutangaza kutowania urais mwaka ujao.
Maandamano hayo yalikuwa yamepigwa marufuku na polisi nchini humo lakini pia serikali imefunga Internet kwa lengo la kuzuia mawasiliano kupitia mitanadao ya kijamii kama facebook na Twitter.
Mbali na wauamini wa Kanisa Katoliki, Mashirika ya kiraia na wanasiasa wa upinzani walikuwa wamepanga kushiriki katika maandamano hayo ya mwisho wa mwaka 2017.
Kiongozi wa upinzani Felix Tshisekedi ambaye alikuwa katika Kanisa la Katoliki la Gombe, Kaskazini mwa jiji hilo, naye alirushiwa mabomu ya kutoa machozi na kusababisha kusitishwa kwa ibada iliyokuwa inaendelea
Kabila ambaye amekuwa akiongoza DRC tangu mwaka 2001, na ambaye kwa mujibu wa serikali ya pamoja muda wake unamalizika leo, hajatangaza iwapo hatawania urais mwakani.
Uchaguzi ulikuwa umepangwa kufanyika mwisho wa mwaka 2017, lakini kwa sababu mbalimbali hasa za kiusalama, Tume ya Uchaguzi ikaahirisha hadi mwaka 2018.