Watu saba wauawa baada ya shambulizi la kigaidi mjini Mogadishu
Watu saba wameuawa na wengine 10 kujeruhiwa mjini Mogadishu nchini Somalia baada ya gari dogo lililokuwa mabomu kulipuka karibu na Mkahawa mmoja unaopakana na Wizara ya Mambo ya ndani.
Imechapishwa:
Wizara ya Usalama imesema mlipuko mkubwa ulisikika karibu na mkahawa huo maarufu kwa kuuza chai Jumatano asubuhi wakati watu wakipata kiamsha kinywa.
Abdifatah Omar Halane msemaji wa Wizara hiyo, amethibitisha kuuawa kwa watu hao saba na kuwajeruhiwa kwa wengine 10.
Magari ya kubeba wagonjwa yalionekana katika eneo hilo baada ya mlipuko huo kwa mujibu wa wale walioshuhudia tukio hilo.
Hadi sasa hakuna kundi lililojitokeza kudai kutekeleza shambulizi hilo.
Hata hivyo, mashambulizi kama haya yamekuwa yakitekelezwa na kundi la kigaidi la Al Shabab ambalo mara kadhaa limekuwa likijaribu kuipindua serikali mjini Mogadishu bila mafanikio.
Al-Shabab waliondolewa katika mji huo Mkuu mwaka 2011.