Mali: vurugu zaongezeka Gao
Katika jimbo la Gao, kaskazini mwa Mali, manispaa ya jiji imepiga marufuku maandamano licha ya kuwa yamefanyika Jumanne hii asubuhi.
Imechapishwa:
Vijana wametikia wito wa mashirika kadhaa ya kiraia wa kuandamana dhidi ya kuanza kazi kwa viongozi wa mpito waliyowekwa kulingana na makubaliano ya Algiers. Wanaomba pia kuingizwa katika jeshi. Mkutano huo uligubikwa na machafuko.
Jumanne mchana, milio ya risasi imekua ikisikika katika mitaa mbalimbali ya mji, kwa mujibu wa wakazi. Maeneo manne kati ya saba ya mji wa Gao yalikumbwa na vurugu.
Vijana kadhaa wameingia mitaani Jumanne asubuhi licha ya kupigwa marufuku na manispaa ya jiji ambayo ilibaini kuwekwa hali ya hatari. Vikosi vya usalam vilitumwa ili kutoa ulinzi katika mitaa ya mji huo. Vijana walirusha mawe, polisi ikajibu kwa kutumia mabomu ya machozi. Kwa mujibu wa mashahidi, askari polisi walianza kurusha risasi za moto, angalau hewani.
Idara ya dharura katika hospitali ya mjini Gao imethibitisha vifo vya watu wawili na wengine 17 kujeruhiwa, ikiwa ni pamoja na wawili wakiwa katika hali mbaya. Kwa mujibu wa mkuu wa Idara hiyo, vijana waliojeruhiwa wamekua wakiendelea kuingizwa kwa wingi hospitalini, na idadi inatarajiwa kuongezeka.
Hali bado ni tete, na mkuu wa jimbo la Gao ametolea wito raia kuwa watulivu.