Hatimaye Salva Kiir na Riek Machar wakubaliana kusitisha mapigano Sudani Kusini
Marekani imepongeza makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyo fikiwa na rais Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar , na kuwataka viongozi hao kutekeleza haraka iwezekanavyo,ahadi zao za kukomesha vita ya wenyewe kwa wenywe iliyodumu kwa karibu miezi mitano.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Msuluhishi mkuu wa mgogoro wa Sudani Kusini kutoka jumuiya ya IGAD Seyoum Mesfin amesema kuwa rais Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar wametia saini makubaliano ya kumaliza vita.
Mahasimu hao wawili , ambao kwanza walishikana mikono na kisha kusali pamoja, wamekubaliana kumaliza mapigano yote ndani ya saa 24 baada ya kusaini makubaliano hayo.
Makubaliano hayo yamefikiwa jana Ijumaa jijini Adis Ababa nchini Ethiopia juma moja baada ya waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani John Kerry kukutana na rais Salva Kiir jijini Juba.
Marekani ambayo ni muungaji mkono mkubwa wa harakati za Sudani Kusini kupata uhuru wake kutoka Khartoum, imekuwa ikipeleka pesa nyingi za msaada nchini Sudani kusini tangu ijitenge na Sudani mwaka 2011,imeshawishi kwa kiasi kikubwa makubaliano yaliyofikiwa.