China yaendelea na jitihada za kupambana dhidi ya virusi vya Corona
China inararajiwa kufungua hospitali mpya inayolenga kutoa matibabu kwa watu waliombukizwa virusi vya Corona, wakati huu idadi ya watu waliombukizwa ikiendelea kuongezeka.
Imechapishwa:
Hospitali hiyo iliyojengwa kwa muda wa siku nane zilizopita, inatarajiwa kufunguliwa katika mji wa Wuhan, eneo ambalo virusi hivyo viliripotiwa kwa mara ya kwanza.
Hatua hii inakuja, wakati huu maafisa wakisema kuwa, idadi ya watu walipoteza maisha kutokana na virusi hivyo, imefikia 361 huku wengine zaidi ya 17,000 wakiambukizwa.
Kwa mara ya kwanza, mgonjwa wa kwanza nje ya China amepoteza maisha nchini Ufilipino, baada ya kuwasili nchini humo akitokea mjini Wuhan hivi karibuni, huku idadi ya watu walioambukizwa nje ya China wakifikia 150.
Mataifa mbalimbali yameendelea kuwazuia watu kutoka nchini China, kuingia katika nchi zao kwa hofu ya kuendelea kusambaa kwa virusi hivyo ambavyo Shirika la afya duniani WHO, linasema sasa ni janga la kimataifa.