Watu karibu ya 100 wauwawa katika machafuko mjini Abyei
Watu wanaokadiriwa kufikia mia moja wameuawa nchini Sudan, katika eneo lenye utajiri wa mafuta la Abyei, wakati Majeshi ya Sudan Kaskazini yalipovamia eneo hilo na kuchangia kuzuka kwa machafuko.Takwimu hizo zimetolewa na Deng Arop Kuol, aliyekuwa Kiongozi wa Abyei kabla ya kutimuliwa kwenye wadhifa wake na Rais wa nchi hiyo Omar Hassan Al-Bashir. Kuol, ameongeza kuwa hali imezidi kuwa mbaya huku wananchi wakihitaji misaada zaidi ya kibinadamu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa upande wa Vikosi vya Umoja wa Mataifa (UN) vinavyoshika doria nchini Sudan kupitia Msemaji wao Hua Jiang, amesema wameendelea kushuhudia maiti mitaani wakati wakiwa kwenye doria zao.
Abyei, ni eneo ambalo, kutokana na utajiri wake wa mafuta- rasilimali muhimu kwa ukuaji wa taifa hilo, limeshuhudia mapigano makali baina ya majeshi ya Kaskazini na Kusini, ambayo kila mmoja inagombania eneo hilo, liwe mali yake.
Kufuatia kadhia hiyo, iliyodumu kwa miaka mingi, hatimaye raia wa Sudan Kusini walipata fursa ya kupiga kura ya maamuzi mnamo tarehe 9 Januari, mwaka huu.
Zoezi hilo lilifanikisha ndoto ya raia wengi wa Sudan Kusini, ambao walisherehekea maamuzi hayo usiku na mchana.