Mtuhumiwa wa shambulio la msikiti New Zealand akana mashtaka dhidi yake
Mtuhumiwa mkuu wa mauaji ya watu 51 aliowapiga risasi wakiwa msikitini kwenye mji wa Christchurch nchini New Zealand mwezi machi mwaka huu, amekana mashtaka yote yanayomkabili.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mwanasheria wa Brenton Tarrant mwenye umri wa miaka 28, amesema mteja wake amekana mashtaka yote 51 ya mauaji, 40 ya jaribio la kuua na moja la kutekeleza kitendo cha kigaidi.
Hii ni mara ya kwanza kwa mashtaka ya ugaidi kusikilizwa kwenye mahakama za New Zealand.
Tarrant mwenyewe hakuwepo mahakamani wakati kesi yake ikisikilizwa lakini alionekana kupitia picha za video kutoka kwenye jela ambako anashikiliwa.
Katika muda wote wa karibu dakika 30, Tarrant hakusema kitu chochote mbali ya wakati mmoja kutikisa kichwa chake kuonesha ishara kuwa alikuwa anamsikia jaji anayesikiliza kesi yake.
Wakati mwanasheria wake amesimama na kusema kuwa mteja wake anakana mashtaka dhidi yake, Tarrant alionekana kuonesha ishara ya kukonyeza kwenye kamera iliyokuwa ikirekodi.
Tarrant ambaye amjipambanua kama mzungu mwenye msimamo mkali, anatuhumiwa kuhusika peke yake katika tukio la Machi 15, ambapo akiwa na bunduki aliingia msikitini na kuanza kuwafyatulia risasi waumini.
Serikali ya New Zealand tayari imepitisha sheria kali dhidi ya wamiliki wa aina ya silaha ambayo ilitumiwa na Tarrant.