Wahamiaji 108 waruhusiwa kuingia Sicily
Meli ya mizigo ya Denmark iliyokua ikibeba wahamiaji 108 waliokolewa Ijumaa wiki iliyopita katika pwani ya Libya, hatimaye iliruhusiwa usiku wa Jumatatu kuamkia Jumanne wiki hii kutia nanga Sicily.
Imechapishwa:
Hata hivyo bado kuna hofu kuhusu hatima ya wahamiaji wengine 234 wanaosafiri na Lifeline, meli iliyokodeshwa na shirika lisilo la kiserikali.
Lifeline, meli iliyokodeshwa na shirika lisilo la kiserikali kutoka Ujerumani imekataliwa kutia naga nchini Italia na kwa sasa imekwama baharini. Waziri wa Mambo ya Ndani wa Italia Matteo Salvini alithibitisha Jumatatu wiki hii hatua yake kali dhidi ya mashirika yasiyo ya kiserikali yanayosaidia wahamiaji.
Meli kutoka Denmark, Alexander Maersk, iliwasili usiku huko Pozzallo, baada ya siku tatu ikisubiri mbele ya bandari hiyo kusini mwa Sicily. Ilibadilisha njia siku ya Ijumaa asubuhi ili kuwaokoa wahamiaji kutoka Libya.
Katika mkutano na waandishi wa habari aliporudi kutoka Libya, Bwana Salvini alisem aakisisitiza kuwa meli ya Lifeline na wahamiaji 234 waliomo hawataruhusiwa kuingia nchini Italia.
Spika wa Bunge la Corse, Jean-Guy Talamoni, alisema siku ya Jumatatu kuwa yuko "tayari kusaidia" wahamiaji waliokwama kwenye meli ya Lifeline. Hata hivyo, aliongeza kwenye redio ya France Inter kwamba "kwa kisheria, kunahitajika makubaliano ya serikali ya Ufaransa ili mambo yaweze kusonga mbele".