Wakuu wa nchi za Ulaya, wataka mchakato wa Uingereza kutoka uharakishwe
Saa chache baada ya waziri mkuu wa Uingereza, David Cameron, kusema kuwa ataondoka madarakani kabla ya mwezi October mwaka huu baada ya kura ya maoni ya kujitoa kwenye umoja wa UIaya, wakuu wa jumuiya hiyo wanataka nchi hiyo isichelewe kutoka.
Imechapishwa:
Baadhi ya wakuu wa nchi za Jumuiya ya Ulaya waliotoa maoni yao kuhusu uamuzi uliofanywa na wananchi wa Uingereza, wanataka mchakato wa Uingereza kuondoka ndani ya Jumuiya yao, usichukue muda mrefu kwani kuendelea kuchelewa kutaathiri ukanda wao.
Mkuu wa tume ya umoja wa Ulaya, Jean-Claude Junker, amesema kuwa licha ya hatua ya wananchi wa Uingereza ambao wanapaswa kuheshimiwa kutokana na uamuzi waliouchukua, nchi 27 wanachama zilizosalia zitaendelea kushirikiana.
Wananchi wa Uingereza wamepiga kura kwa asilimia 52 kujitoa kwenye umoja wa Ulaya, huku asilimia 48 wakitaka kutojitoa kwenye umoja huo, uamuzi ambao sasa ni wazi umemfanya waziri mkuu David Cameron kibarua chake kutamatika hata kabla ya muda.
Akizungumza kwa uchungu baada ya kutangazwa kwa matokeo rasmi, waziri mkuu Cameron, amesema kuwa jukumu la kutenguliwa na azimio namba 25 la mkataba wa nchi hiyo kuwepo kwenye Jumuiya ya Ulaya, ni jukumu la waziri mkuu ajaye.
Saa chache baada ya kutangazwa kwa matokeo ya kura hiyo ya maoni, tayari sarafu ya Paundi ya Uingereza imeporomoka na masoko ya hisa kwenye nchi mbalimbali yametikisika.
Rais wa Ufaransa, Francois Hollande na kansela wa Ujerumani Angela Merkel, wamekosoa hatua ya nchi ya Uingereza kujitoa kwenye umoja wa Ulaya, kwa kile walichosema walikuwa wanaamini kuwa Uingereza ingestawi kama ingeendelea kuwa nchi mwanachama.
Kwa upande wake waziri mkuu wa Scotland, Nicola Sturgeon, amesema nchi yake itafanya kura nyingine ya maoni kujiamulia ikiwa wasalie ndani ya umoja wa Ulaya ama watoke.
Mgombea urais wa Marekani anayewania kuteuliwa na chama chake cha Republican, Donald Trump, amewapongeza wananchi wa Uingereza kwa kile alichosema wameamua kurejea nchi yao kutoka kwa wanyonyaji na kwamba nchi nyingine zifuate mfano wa Uingereza.
Kinara wa kampeni ya Uingereza kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya, Boris Johnson akizungumza mara baada ya matokeo kutangazwa, amesema huu ni ushindi kwa wananchi wa Uingereza, na ni ishara tosha kuwa wameamua kubaki na nchi yao.
Kujitoa kwa nchi ya Uingereza kwenye umoja wa Ulaya, pia kumeungwa mkono na mkurugenzi wa shirika la fedha duniani IMF, Christine Lagarde ambaye ameunga mkono hatua zilizotangazwa na gavana wa benki kuu ya Uingereza, kuhusu namna itakavyoshughulikia sarafu ya nchi hiyo ili kuhakikisha uchumi wake hautetereki.
Wachambuzi wa mambo wanaona kuwa uamuzi huu wa nchik ya Uingereza unaofanyika miaka 40 toka ilipojiunga, umezusha hofu ya kufanyika kwa kura nyingine za maoni kwenye baadhi ya nchi kama vile, Ugiriki na Italia ambazo awali ziligusia kufanya kura ya maoni.