Mazungumzo ya kusaka suluhu nchini Syria, kati ya Serikali na upinzani yaanza rasmi mjini Geneva
Mazungumzo ya kusaka amani ya kudumu nchini Syria kati ya pande zinazohasimiana nchini humo, yameanza rasmi hapo jana mjini Genava, huku mjumbe maalumu wa umoja wa Mataifa akieleza matumaini ya kuzileta pamoja pande hizo.
Imechapishwa:
Akizungumza mara baada ya kuwa na mazungumzo ya awali na upande wa upinzani, balozi Staffan de Mistura amesema kuwa mazungumzo ya ana kwa ana kati ya Serikali na upinzani sasa yameanza rasmi.
Mwanadiplomasia huyu mwenye asili ya Sweden na Italia, amesema anatarajia mazungumzo kuwa magumu, lakini anaamini kuwa wananchi wa Syria wanastahili kupata mwanga mzuri baada ya kushuhudia miaka kadhaa ya maumivu na mauaji.
De Mistura hakusema moja kwa moja ni muda gani mazungumzo haya ya awali yatachukua lakini akaongeza kuwa ni matarajio yake mpaka kufikia February 11 wajumbe wa pande zote mbili watakuwa wameafikiana kitu.
Upande wa upinzani ambao uliwasili mjini Geneva toka Jumamosi ya wiki iliyopita, wamekuwa wakisuasua kushiriki kwenye mazungumzo haya ya karibu miezi sita na kukutana ana kwa ana na viongozi wa utawala wa Syria.
Kundi hilo la upinzani limetaka kabla ya kuanza kwa mazungumzo yenyewe, misaada ya kibinadamu ipelekwe kwenye miji yenye mapigano na pia nchi ya Urusi na Serikali ziache mara moja kushambulia maeneo hayo pamoja na kuwaachia huru wafungwa wa kivita.
Katika kile kianchoonekana ni mwanzo mzuri kwa ujumbe wa Serikali ya Syria, utawala huo ulikubali hapo jana kupelekwa kwa misaada kwenye mji wa Madaya na miji mingine inayokabiliwa na mapigano.
Hapo jana wataalamu wa masuala ya mizozo wameonya kuhusu kutolewa kwa masharti na upinzani kabla ya kushiriki mazungumzo yenyewe hali wanayosema huenda ikakwamisha mazungumzo yanayoanza.