EU : Kansela wa Ujerumani atoa wito kwa nchi wanachama kuisaidia zaidi Ukraine
Nairobi – Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz, ametoa wito kwa nchi wanachama wa EU na Marekani kufanya juhudi zaidi kusaidia nchi ya Ukraine inayokabiliwa na uvamizi wa Urusi.
Imechapishwa:
Wito wake umekuja kuelekea ziara yake jijini Washington kwa ajili ya mazungumzo na rais Joe Biden.
Akizungumza wakati akiwa Berlin, Scholz ameeleza kuwa msaada unaotolewa na washirika wa Kyiv katika vita vyake dhidi ya Moscow bado hautoshi.
Ziara ya Scholz katika nchi mshirika wake muhimu imekuja wakati huu msaada wa Dolla Bilioni 60 uliopendekezwa na rais Joe Biden kwa Kyiv ukionekana kukwama katika bunge la senate nchini Marekani kutokana na mvutano kati ya maseneta wa Republican.
Viongozi wa Umoja wa Ulaya wiki iliopita walikubaliana kuidhinisha msaada wa Dolla Bilioni 50 kwa nchi ya Ukraine baada ya kukabiliwa na upinzani wa miezi kadhaa kutoka kwa kiongozi wa nchi ya Hungary Viktor Orban.
Scholz anatarajiwa kuanza ziara yake nchini Marekani siku ya Alhamis ambapo atakuwa na mazungumzo na rais Joe Biden.