Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Blinken kuzuru Korea Kusini
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken atazuru Korea Kusini wiki ijayo kwa majadiliano kuhusu masuala muhimu ikiwa ni pamoja na Korea Kaskazini yenye silaha za nyuklia, wizara ya mambo ya nje ya Seoul imethibitisha.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Blinken anatarajiwa kuwasili jijini Seoul Jumatano ijayo kwa safari ya siku mbili, ikiwa ni ziara yake ya kwanza nchini humo tangu Machi 2021.
Waziri huyo wa mambo ya kigeni wa Marekani atakutana na mwenzake wa Korea Kusini Park Jin kwa ajili ya mazungumzo kuhusu mambo mengi tu ikiwemo masuala ya Korea Kaskazini, usalama wa kiuchumi na teknolojia ya hali ya juu, pamoja na hali ya kikanda na kimataifa.
Ziara yake Blinken pia inatarajiwa kutoa fursa muhimu ya kuendeleza zaidi ushirikiano wa Korea Kusini na Marekani.
Ziara hiyo inakuja wakati huu Seoul na Washington zikiimarisha ushirikiano wa kiulinzi katika kukabiliana na mfululizo wa majaribio ya silaha yaliofanywa na Pyongyang mwaka huu.
Aidha ziara hii pia inakuja wakati huu uhusiano wa Korea Kaskazini na Urusi ukionekana kuendelea kuimarika hali ambayo imezua hofu kwa nchi za Magharibi kwamba Pyongyang inaipatia Moscow silaha kwa ajili ya vita vyake nchini Ukraine.
Viongozi wa nchi hizo, Kim Jong Un na Vladimir Putin, mwezi Septemba walifanya mkutano nchini Urusi, waziri wa mambo ya nje wa Moscow Sergei Lavrov, akitarajiwa kuzuru Pyongyang mwezi ujao.