Kim Jong Un anaendelea na ziara yake nchini Urusi
Nairobi – Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un ametembelea kiwanda kikubwa cha Urusi kinachotengeneza ndege za kivita, na vifaa vya angani huku akionyesha kushangazwa na mifumo ya kisasa inayotumiwa na wataalamu wa Urusi.
Imechapishwa:
Cheza - 01:18
Akiwa ziarani huko Urusi Kiongozi huyo wa Korea Kaskazini Kim Jong Un punde baada ya kuwa na mazungumzo ya kina na mwenyeji wake wa Urusi Rais Vladimir Putin, Kim amepata fursa ya kutembelea kiwanda kikubwa kinachotengeneza ndege za kivita, na vifaa vya angani na hakusita kuonyesha kuwa ameshangaa kushuhudia teknolojia na mifumo ya kisasa inayotumiwa na wataalamu wa Urusi.
Kim Jong Un ameviambia vyombo vya habari kuwa wameafikia makubaliano ya kuipatia silaha Urusi katika vita vyake na Ukraine, hatua ambayo ilikashifiwa vikali na Marekani pamoja na Umoja wa Mataifa kabla hata ya kiongozi huyo wa Korea Kaskazini kuanza ziara yake huko Vladivostok.
Hata hivyo hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa kuhusu uwezekano wa Korea Kaskazini kuipatia silaha Urusi.
Siku mbili baada ya kukutana na Putin kwenye kituo cha anga za juu, huku kukiwa na uvumi kwamba wangekubali mkataba wa silaha, treni ya Kim ya kuzuia risasi iliwasili Komsomolsk-on-Amur, vyombo vya habari vya Urusi vimeripoti.
Msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov alisema jana Alhamisi, kwamba Ziara ya Kim itaendelea siku chache zaidi, bila kutoa maelezo zaidi.