Duru ya pili ya uchaguzi wa urais inatarajiwa kufanyika nchini Uturuki
NAIROBI – Duru ya pili ya uchaguzi wa urais inatarajiwa kufanyika nchini Uturuki, baada ya wagombea wakuu rais Recep Tayyip Erdogan na mpinzani wake mkuu Kemal Kilicdaroglu kuonekana kutopata ushindi unaohitajika.
Imechapishwa:
Cheza - 00:54
Tume ya Uchaguzi inasema mpaka sasa, rais Erdogan amepata asilimia 49.49 ya kura huku mpinzani wake Kilicdaroglu akipata asilimia 44.79, wakati huu karibu kura zote zikiwa zimehesabiwa.
Ili kutangazwa mshindi, mgombea anapaswa kupata asilimia 50 na kwa mujibu wa matokeo haya, wapiga kura wanatarajiwa kupiga tena kura baada ya wiki mbili.
Wapinzani wote hao wawili wanasema, wako tayari kwa marudio ya uchaguzi huo, huku kila mmoja akisema, ana uhakika wa kupata ushindi.
Erdogan akizungumza akiwa jijini Ankara, amewaambia wafuasi wa chama chake cha AK kuwa, bado anaamini kuwa atapata ushindi huku Kilicdaroglu akisema Waturuki wameonesha kuwa hawaitaki serikali iliyo madarakani.
Uchaguzi huu umeelezwa kuwa na ushindani mkali, na umefanyika katika kipindi ambacho nchi hiyo inapitia kipindi kigumu cha kiuchumi na janga la matetemeko ya radhi yaliyotokea katika miezi iliyopita.