EU yasitisha makubaliano ya kuwezesha visa kwa Warusi
Nchi 27 wanachama wa Umoja wa Ulaya, ambazo mawaziri wake wa mambo ya nje wamekutana mjini Prague siku ya Jumanne na Jumatano, zimekubali kusitisha kikamilifu makubaliano ya kuwezesha visa ambayo yamekuwepo kati ya EU na Urusi tangu mwaka 2007.
Imechapishwa:
Sehemu ya makubaliano haya na Moscow ilikuwa tayari imesimamishwa kwa baadhi ya watu, wakiwemo wanasiasa na wafanyabiashara.
Maelewano yaliyopatikana Prague Jumatano Agosti 31 yanaongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya raia wa Urusi ambao hawataweza tena kupata visa vya utalii kwa urahisi na haraka katika nchi zote za eneo la Schengen.
Josep Borrell, mkuu wa diplomasia ya Ulaya, amesema mawaziri waliokutana Prague wamekubaliana kwamba uhusiano na Moscow "hauwezi kubaki bila kubadilika" na kwamba makubaliano, yaliyofikiwa mwaka 2007, yanapaswa "kusitishwa kabisa".
'Hatari za usalama'
Kufuatia mkutano wa Prague, alisema kusimamishwa kutafanya upatikanaji wa visa kwa raia wa Urusi "kuwa ngumu zaidi" na "muda mrefu zaidi". "Hii itapunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya visa mpya iliyotolewa na mataifa wanachama wa EU," ameongeza.
Ufini, Poland, nchi za Baltic na Jamhuri ya Czech, hasa, zilikuwa zimeomba kupigwa marufuku kabisa kwa visa zote za watalii. Wakuu wa diplomasia nchini Estonia na Latvia wametilia shaka "hatari za usalama" na wanapanga kuchukua hatua katika ngazi ya kitaifa.
Makubaliano yaliyofikiwa leo bado yanahitaji kuidhinishwa rasmi mjini Brussels. "Hii ni ishara kwa viongozi wa Moscow na Sankt-Peterburg (St. Petersburg) (…) Ninaamini kwamba tutaweza kupendekeza hatua nyingine,” amesema Waziri wa Czech Jan Lipavsky, ambaye nchi yake kwa sasa ni mwenyekiti wa Baraza la EU.