Raia wa Morocco anayeshtumiwa kuwa na uhusiano na IS akamatwa Barcelona
Polisi wa Uhispania wametangaza leo Ijumaa kuwa wamemkamata huko Barcelona raia wa Morocco, anayetajwa kama mtu mwenye itikadi kali za kidini, ambaye anashtumiwa kuwa na uhusiano na kundi la Islamic State, IS.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Polisi ya Uhispania imebaini kwamba raia huyo wa Morocco alikuwa anapanga kufanya shambulio, kufuatia uchunguzi wa pamoja uliofanywa na Morocco na Marekani.
"Mtuhumiwa alikuwa anapanga kutekeleza kitendo cha kigaidi, lakini kufikia sasa haijajulikani ni wapi au lini" , polisi imesema katika taarifa.
Uhusiano wake na kundi la Islamic State, IS, ulianza tangu zaidi ya miaka minne, lakini alianza kuonyesha dalili za nje za itikadi kali hivi karibuni, polisi imebaini.
Uhusiano wake na kundi la Islamic State uliongezeka baada ya ya kutangazwa vizuizi vya kuthibiti maambukizi ya Corona Machi 14 nchini Uhispania kama sehemu ya mapambano dhidi ya janga la Covid-19, taarifa ya polisi imeongeza.
Tangu wakati huo alionyesha hadharani kuwa na uhusiano na kundi la IS, baada ya kutangaza kwenye mitandao ya kijamii kwamba ana chuki na nchi za Magharibi, na alifanya safari kadhaa za siri kwenda Barcelona, ambapo polisi wanaamini alikuwa akikagua baadhi ya maeneo kwa ajili ya shambulio.