Mbivu na mbichi katika taji la klabu bingwa Uingereza kujulikana jumatatu.
Mchuano wa kuwania taji la klabu bingwa nchini Uingereza,kati ya mabingwa watetezi Manchester United na Manchester City siku ya Jumatatu unasubiriwa kwa hamu kubwa huku wadadisi wa soka wakitathmini namna utakavyokuwa.
Imechapishwa:
Utakuwa ni mchuano wa kihistoria ambao utabaini bingwa wa ligi hiyo wakati kukiwa kunasalia michuano miwili kabla ya kumalizika kwa ligi hiyo.
Manchester United inaongoza msururu wa ligi kwa alama 83 huku Manchester City ikiwa ya pili kwa alama 80 baada ya mechi 35 .
Ikiwa Manchester United itashinda mechi hiyo watatawazwa mabingwa wa ligi hiyo kwa mara ya 20 na ikiwa Manchester City watashinda, wataongoza ligi hiyo kwa wingi wa mabao na watahitaji ushindi wa mchuano mmoja kunyakua taji hilo.
Makocha wa vilabu vyote viwili,Mancherster United Sir Alex Ferguson na Roberto Mancin wa Manchester City wanasema kuwa mchuano huo ni muhimu sana katika ukufunzi wao na historia ya timu hizo mbili.
Katika historia ya timu hizo mbili,Mancheter United wameshinda mara 67,wakati Manchester City wakiandikisha ushindi rekodi mara 44.
Timu hizo mbili zimekwenda sare mara 50.
Mara ya mwisho kwa vilabu hivi viwili kukutana ilikuwa mwezi wa kumi mwaka jana,mechi ambayo Manchester City iliishinda Manchester United kwa mabao 6 kwa 1.