Mashirika ya kiraia yahoji kuhusu kiwango cha vurugu katika kampeni za uchaguzi Uganda
Machafuko yaliyotokea mapema wiki hii nchini Uganda baada ya kukamatwa kwa mmoja wa viongozi wa upinzani nchini humo Bobi Wine yameendelea kuzua hali ya sintofahamu nchi himo.
Imechapishwa:
Mashirika ya kiraia yanasema machafuko hayo yanaonyesha kwamba mazingira ya uchaguzi wa urais wa Januari 2021hayatokuwa mazuri.
Kulingana na ripoti ya polisi watu 37 waliuawa na wengi zaidi ya 45 walijeruhiwa vibaya katika makabiliano hayo na wafuasi wa upinzani.
Hayo yanajiri wakati mwanasiasa wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa rais Yoweri Kaguta Museveni, Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine yuko huru tangu jana Ijumaa, Novemba 20 baada ya kuzuiliwa kwa muda wa siku mbili.
Alikamatwa Jumatano wakati akifanya kampeni kabla ya uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika Januari 2021, akishtumiwa kwa kukiuka miongozo ya kudhibiti ugonjwa wa virusi vya corona kwenye mkusanyiko wa hadhara.
Habari za kukamatwa kwake zilizusha maandamano makubwa siku ya Jumatano, lakini vikosi vya usalama vimeshtumiwa kutumia nguvu kupitra kiasi kwa kuvunja maandamano hayo.