Wafanyakazi watatu wa shirika lisilo la kiserikali wakamatwa Burundi
Hali ya sintofahamu yaendelea kujitokeza nchini Burundi baada ya serikali ya Burundi kuchukuwa hatua ya kusitisha shughuli za mashrika yasiyokuwa ya kiserikali. Hayo yanajiri wakati baadhi ya wafanyakazi wa mashirika hayo wameanza kukabiliwa na hatua ya serikali.
Imechapishwa:
Wafanyakazi wataturaia mmoja kutoka DRC na Warundi wawili wamekamatwa katika ofisi ya shirika lisilo la kiserikali la kigeni la IRC, mkoani Muyinga, Kusini mashariki mwa Burundi.
Wafanyakazi watatu wa shirika la IRC (International Rescue Comittee) walikamatwa siku ya Jumatano wiki hii kwa kukiuka marufu iliyowekwa dhidi ya mashirika yasiyo ya kiserikali ya kigeni nchini humo tangu Oktoba 1, serikali ya Burundi imetangaza Alhamisi wiki hii.
Wafanyakazi watatu wa IRC walikamatwa siku ya Jumatano kwa agizo kutoka kwa mkuu wa wilaya, wakati serikali imepiga marufu kwa mashirika hayo kuendelea na shughuli zao hapa nchini," msemaji wa Wizara ya Usalama wa Umma, Pierre Nkurikiye ameviambia vyombo vya habari leo Alhamisi.
"Wote walikuwa kazini bila kibali maalum , kwa sasa wanahojiwa," Bw Nkurikiye amesema, akiongeza kuwa wafanyakazi hawa watatu, raia mmoja kutoka DRC na Warundi wawili, walikamatwa katika ofisi za IRC huko Muyinga.
Taarifa hii ya kukamatwa kwa wafanyakazi hao imethibitishwa na vyanzo vya kidiplomasia na kiutawala. IRC, mojawapo ya mashirika yasiyo kuwa ya kiserikali imekataa kueleza chochote kuhusiana na taarifa hii.
Baraza la Usalama la Taifa la Burundi liliamua mwishoni mwa mwezi Septemba kusitisha kwa miezi mitatu shughuli za mashirika yasiyo ya kiserikali ya kigeni nchini humo mpaka pale yatatekeleza sheria mpya inayodhibiti shughuli zao nchini.