Kesi dhidi ya wanajeshi 13 wa Sudan Kusini yaanza jijini Juba
Kesi dhidi ya wanajeshi 13 wa Sudan Kusini kuhusu madai ya mauaji na ubakaji dhidi ya wafanyikazi watano wa Mashirika Kimataifa ya kutoa misaada ya kibinadamu mwaka uliopita imeanza katika Mahakama ya kijeshi jijini Juba.
Imechapishwa:
Mwandishi wa RFI Kiswahili James Shimanyula ameripoti kesi hiyo kuanza chini ya ulinzi mkali jijini Juba.
Mmoja wa Mashahidi katika kesi hiyo Michael Woodward, ambaye ni Mkurugenzi wa Hoteli ya Terrain, ameiambia Mahakama hiyo ya kijeshi kuwa wanajeshi hao walibomoa milango ya maakazi ya wafanyikazi hao na kuwabaka.
'Waliwabaka wanawake watano wanaofanya kazi na mashirika ya kimataifa yanayotoa misaada ya kibinadamu. Walifyatua risasi hapa na pale na kupora mali,” alisema Woodward.
Naye kiongozi wa Mashtaka Kanali Abubaker Mohamed Ramadhan amesema kesi hiyo imeanza vizuri, na inatoa matumaini kuwa haki itapatikana.
“Ni mwanzo mzuri wa kesi kwani kesi hii imekuwepo kwa zaidi ya mwaka mmoja na Jumuiya ya Kimataifa imekuwa ikisubiri matokeo ya kesi hii,” amesema Kanali Ramadhan.
Wanajeshi hao 13 wanawakilishwa na Wakili kutoka jijini Juba ambaye pia ni mwajeshi Luteni Peter Malwal Deng ambaye ameanza kuwahoji mashahidi kutoka upande wa Mashtaka.
Vikosi vya Sudan Kusini vimekuwa vikituhumiwa kutekeleza mauaji ya raia tangu kuzuka kwa vita nchini humo mwaka 2013.