UN: Mamilioni ya raia wanahitaji msaada wa chakula Sudani Kusini
Zaidi ya robo tatu ya wananchi wa Sudani Kusini wanakabiliwa na njaa, wakati huu taifa hilo lililokumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe likiwa hatarini kukumbwa na baa la njaa, imesema taarofa ya umoja wa Mataifa na Serikali ya Juba.
Imechapishwa:
Licha ya mkataba wa amani kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe, watu wanaokadiriwa kufikia milioni tano, ikiwa ni zaidi ya ilivyowahi kushuhudiwa kwenye taifa hilo jipya kabisa duniani, wanahitaji chakula kuishi.
Ripoti hii inatolewa wakati ambapo, maelfu ya raia wameendelea kukimbia kwenye mji wa Wau wakihofia kuuawa kutokana na mapigano yaliyozuka mwishoni mwa juma lililopita, huku Serikali ikishindw akabisa kudhibitia uasi unaoendelea kwenye eneo hilo.
Wafanyakazi wa misaada wamefanikiwa kufika kwenye baadhi ya maeneo ambayo yanakabiliwa na hali mbaya ya chakula, lakini kuendelea kwa mapigano kati ya makundi yenye silaha ambayo hayaheshimu Serikali, yanatatiza shughuli za misaada.
Shirika la kilimo duniani FAO linasema hali ya uhaba wa chakula kwa mwaka huu ni mbaya, kwenye taarifa iliyotolewa kwa pamoja na shirika la mpango wa chakula WFP na linalohusika na watoto UNICEF.
Taarifa hiyo inasema zaidi ya watu milioni 4 na laki 8 nchini Sudani Kusini watakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula katika miezi ijayo, na kuonya kuhusu uwezekano wa nchi hiyo kukumbwa na baa la njaa.