DRC: Rais Tshisekedi aapishwa kuongoza muhula wa pili
Nairobi – Rais Felix Thisekedi ameapishwa siku ya Jumamosi kuongoza Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, kwa muhula wa pili, baada ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi mkuu uliofanyika mwezi Desemba mwaka uliopita.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mbele ya maelfu ya wananchi na marais mbalimbali wa mataifa ya Afrika, Tshisekedi ameapa kuheshimu na kuitetea katiba na kuulinda uhuru wa DRC.
“Naapa kulinda heshima na mipaka ya nchi yetu,” alisema mbele ya maelfu ya watu na wageni mashuhuri kwenye uwanja wa Martyrs jijini Kinshasa.
Tshisekedi katika hotuba yake, amesema anafahamu kuwa wananchi wa taifa hilo wana matarajio makubwa na uongozi wake.
Ameahidi kupambana na utovu wa usalama Mashariki mwa nchi hiyo na kupambana na janga la ukosefu wa ajira hasa kwa vijana pamoja na kuhakikisha uwiano wa nchi.
Ushindi wa Tshisekedi, umeendelea kupingwa na wanasiasa wa upinzani, wakiongozwa na Moise Katumbi aliyemaliza wa pili na Martin Fayulu, waliotisha maandamano ya nchi nzima siku ya uapisho kutaka matokeo yaliyomrejesha madarakani, rais huyo kufutwa.
Hata hivyo, jijini Kinshasa kama ilivyokuwa kwenye miji mingine, maandamano hayo hayakufanyika , toafauti na Goma ambapo baadhi ya wafuasi wa upinzani walijitokeza kupinga kuapishwa kwa Thisekedi.