Karimu Khan: Mwendesha mashtaka wa mahakama ICC amezuru Bukavu DRC
NAIROBI – Mwendesha mashtaka Mkuu wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu ICC Karim Khan, anafanya ziara mjini Bukavu Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambapo jana alikutana na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel ya 2018 daktari Denis Mukwege na kujadiliana mbinu mpya za kukabiliana na visa vya uhalifu wa kivita katika eneo hilo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Alfonsine Munganga ni miongoni mwa raia waliojitokeza wakiwa na nia ya kumueleza kiongozi huyo masaibu yaliyompata mwaka 2017 kule Kalehe.
“Tutendewe haki kama tunavyoomba. Tunapenda amani. Nilipokuwa mchuuzi wa Mkaa nilikutana na watu walionitendea mabaya kisha nikaletwa huku.”alisemaAlfonsine Munganga.
Alfonsine Munganga, Raia wa DRC
Mwendesha mashtaka Mkuu wa ICC Kharim Khan amehakikishia wahanga wa vitendo vya kihalifu kwamba mahakama hiyo itachukua hatua dhidi ya waliohusika na vitendo hivyo.
"Ni wakati wa kufanya kazi pamoja ili watoto hawa ambao nimewaona hivi punde, ambao walizaliwa na mabinti wenye umri mdogo pia, wawe kizazi cha mwisho kupitia kile mlichopitia. Ni rahisi kuzungumza-zungumza, na tumekuwa tukizungumza juu ya hili tangu 2004. Nadhani wakati umepita wa maneno-maneno. lazima tuchukue hatua na kufanya kazi pamoja, kwa ajili ya watu wa DRC, na watoto wenu” alisema Mwendesha mashtaka Mkuu wa ICC Kharim Khan.
Mwendesha mashtaka Mkuu wa ICC Kharim Khan
Pia Karim Khan aliwasikiliza wanawake wawili kutoka vijiji vya Kaziba na Katogota vilivyo shambuliwa na watu wenye silaha mnamo miaka ya 1996 na 2000, wakimkumbusha pia hali ya usalama inavyozorota kwa sasa katika jimbo jirani la kivu ya kaskazini.
Kwa sababu mahakama ya kimataifa haiwezi kufuatilia makosa ya uhalifu yaliotekelezwa kabla ya kuundwa kwake mnamo mwaka 2002, Daktari Mukwege na miungano kadhaa wametoa wito wa kuundwa kwa Mahakama maalum ya kimataifa inayoweza kusikiliza na kuchunguza makosa ya uhalifu uliotekelezwa zamani.