Kenya : Kura ya maoni yaonesha Raila anaongoza kwa umaarufu
Utafiti wa shirika la Infotrak unashiria kuwa iwapo uchaguzi ungefanyika hii leo nchini Kenya , mgombea urais wa Azimio la Umoja-One Kenya, Raila Odinga angeongoza katika kaunti 20 na kupata takriban kura 9.3 milioni huku mpinzani wake mkuu Naibu Rais Dkt William Ruto akiibuka mshindi katika kaunti 16 na kujizolea takriban kura 8.4 milioni.
Imechapishwa:
Kulingana na utafiti huo, Raila na mgombea mwenza wake Martha Karua wanaongoza kwa asilimia 42 huku mgombea urais wa Kenya Kwanza Dkt Ruto na mgombea mwenza wake Rigathi Gachagua wakipata jumla ya asilimia 38.
Utafiti huo uliofanyika katika kaunti zote 47 kati ya Mei 27 na 29 unaashiria kuwa umaarufu wa Dkt Ruto umeshuka kutoka asilimia 42 hadi 38 huku umaarufu wa Bw Odinga ukisalia vilevile, amesema mkurugenzi wa Infotrak Bi Angela Ambitho.
kinyume na utafiti wa Infotrack, utafiti wa shirika la Intel Research Solutions, ulitolewa jumanne ulionesha naibu rais wa taifa hilo William Ruto anaongoza kwa umaarufu wa asilimia 49. 9 dhidi Raila odinga ambaye ana asilimia 42.5, kuelekea uchaguzi wa Agosti tisa.
Kura za maoni nchini Kenye hata hivyo huwa hazitiliwi maanani sana na raia, kuelekea uchaguzi wa Agosti 9.