Kundi la waasi wa zamani la Seleka laapa kuendelea na harakati zake za kushikilia baadhi ya maeneo Jamhuri ya Afrika ya Kati
Machafuko baina ya pande za kidini zinazohasimiana nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati yamesababisha mauwaji ya watu wapatao 75 katika makabiliano ya hivi karibuni. Wapiganaji wa zamani Seleka walioondolewa kwenye ngome yao mjini Sibut na askari wa Ufaransa na wale wa Misca wamedai kuelekea sasa maeneo ya Kaga-Bandoro na Bambari Kusini mwa mji huo ili kujipanga upya.
Imechapishwa:
Kamanda wa Waasi wa Seleka walioondolewa mjini Sibut, Kanali Yunus Ayat, amesema bado wataendelea na harakati zao hasa kushikilia baadhi ya maeneo ya kaskazini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati.
“Tunaendelea na mazoezi yetu pembezoni mwa mji wa Sibut, hatuko mjini lakini tuko nje kidogo ya mji. Kati yetu wako wa FAKA tangu zama za Ange Felix Patasse na Francois Bozize, lazima tupambane, eneo la kaskazini ni letu na lazima tulimiliki hata ikitupasa kufa”, amesema Ayat .
Wakati hayo yakijiri, Waziri wa mambo ya Nje wa Ufaransa Laurent Fabius anatarajia kumpokea balozi wa nchi ya Marekani kwenye Umoja wa Mataifa, Samantha Power , kwa majadiliano zaidi juu ya Jamhuri ya Afrika ya Kati, Syria na Mali.
Jumuiya ya kimataifa hivi karibuni, ilimtaka rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Michel Djotodia na waziri wake mkuu Nicolas Tiangaye kujiuzulu, wakiwashutumu kwamba walishindwa kukomesha machafuko.
Machafuko nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati yamesababisha maelfu ya watu kupoteza maisha na wengine zaidi ya 400,000 kuyahama makaazi yao.