Pata taarifa kuu
MISRI-EU

Catherine Ashton athibitisha kuwa kiongozi wa Misri aliyeondolewa madarakani yuko salama

Mkuu wa Sera za mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya EU, Catherine Ashton amekutana na Rais wa Misri aliyeondolewa madarakani, Mohamed Morsi wakati huu ambapo wafuasi wake wameendelea na maandamano jijini Cairo. Vyanzo vya habari nchini humo vimesema kuwa Ashton amekutana na Morsi ambaye hajawahi kuonekana hadharani tangu alipopinduliwa tarehe 3 mwezi Julai.

REUTERS/Egyptian Presidency/Handout via Reuters
Matangazo ya kibiashara

Msemaji wa Ashton Maja Kocijancic amesema kiongozi huyo amezungumza na Morsi kwa masaa mawili mfululizo katika eneo la siri ambalo kiongozi huyo amehifadhiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Cairo, Ashton amesema Morsi yupo salama na anaendelea vizuri huku akiwaeleza wafuasi wake na familia yake kutokuwa na hofu juu ya usalama wa kiongozi wao.

Aidha kiongozi huyo amesema ameweza kuzungumza vizuri na Morsi kwani anafahamu juu ya hali ya mambo inavyoendelea kwani amekuwa akifuatilia taarifa kupitia televisheni na magazeti.

Hata hivyo Mjumbe huyo wa EU hajaweka wazi juu ya mazungumzo yao na kueleza kuwa alimuhakikishia Morsi kuwa hataweka hadharani ajenda za mazungumzo yao.

Ashton aliyewasili jijini Cairo mwishoni mwa juma lililopita amekuwa na mazungumzo na viongozi kadhaa wa Taifa hilo akiwamo Rais wa serikali ya mpito Adly Mansour, Makamu wa Rais katika wizara ya mambo ya nje Mohamed ElBaradei, Mkuu wa Jeshi Generali Abdel-Fattah al-Sisi na wawakilishi wa chama cha Morsi cha Muslim Brotherhood.

Hofu ya usalama imeendelea kutanda nchini humo hasa mara baada ya mauaji ya watu zaidi ya sabini mwishoni mwa juma lililopita.

Maandamano ya wanaomuunga mkono Morsi yameendelea kufanyika ambapo waandamanaji walizunguka ofisi za usalama, ingawa kulitolewa onyo kwa waandamanaji kutotumia vibaya haki yao ya kuandamana.

Mashirika yasiyo ya kiserikali yametoa ombi la kutaka Waziri wa mambo ya ndani wa nchi hiyo, Mohamed Ibrahim atimuliwe kazi na kushtakiwa kutokana na kushindwa kudhibiti mauaji hayo.

Walinda usalama nchini humo bado wanashutumiwa kutumia silaha nzito dhidi ya waandamanaji, taarifa ambazo zimeendelea kukanushwa na wizara ya mambo ya ndani wakidai hutumia mabomu ya kutoa machozi pekee katika kutawanya waandamanaji.

Hivi karibuni Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon aliitaadharisha serikali ya mpito kuwa mauaji ya waandamanaji nchini humo yanakwamisha juhudi za kutatua mgogoro huo unaoendelea kutatiza nchi hiyo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.