Pata taarifa kuu
JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA CONGO

Jeshi la Serikali Nchini DR Congo FARDC limeendelea kushambulia ngome za Kundi la Waasi la M23 kwa kutumia Helkopta tatu za Kijeshi

Jeshi nchini jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo FARDC limejigamba kuendelea kushambulia ngome za Kundi la Waasi la M23 zilizopo Mashariki mwa Taifa hilo karibu kabisa na Mji wa Goma wakiotumia helkopta tatu za kijeshi. Taarifa za kijeshi zimeweka bayana helkopta tatu za kijeshi zimeendelea kurusha mabomu kwenye ngome za Kundi la M23 bila ya wapiganaji wa kundi hilo kujibu mashambulizi hayo kitu kinachoashiria wamefanikiwa kuwasambaratisha.

Wanajeshi wa Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo FARDC wakiwa kwenye doria huko Kivu Kaskazini
Wanajeshi wa Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo FARDC wakiwa kwenye doria huko Kivu Kaskazini REUTERS/Kenny Katombe
Matangazo ya kibiashara

Mashambulizi hayo ya Jeshi la Serikali la FARDC kwa kutumia helkopta za kijeshi ni ya kwanza kufanyika mapema leo asubuhi baada ya kuzuka kwa mapigano makali hiyo jana katika Mji wa Kibati na kuchangia maelfu ya wananchi kukimbia makazi yao kueleka Goma.

Hofu imeendelea kutanda Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC kutokana na kuzuka kwa mapigano mapya kati ya Jeshi la Serikali la FARDC na Wapiganaji wa Kundi la Waasi la M23 karibu kabisa na Mji wa Goma na kuchangia maelfu ya wananchi kukimbia makazi yao.

Mapigano hayo yamezuka baada ya kuwepo wa utulivu wa siku nne kitu ambacho kimechangia kuwepo kwa kurushiana kwa maneno baina ya Jeshi la FARDC na Kundi la Waasi la M23 ambapo kila upande umekuwa ukilaumu wenzao kuhusika na kuanzishwa kwa vita hivyo.

Maofisa wa Jeshi la Serikali la FARDC wamethibitisha Wapiganaji wa Kundi la Waasi la M23 ndilo lilianza kurusha makombora kulenga kambi zao kitu kilichowasukuma nao kujibu mashambulizi hayo na hivyo kuzuka upya kwa mapigano makali katika Mji wa Kibati.

Msemaji wa Kijeshi wa Kundi la Waasi la M23 Kanali Vianney Kazarama amepeleka lawama kwa Jeshi la FARDC kuwa ndiyo lilianza kurusha mabomu wakitumia ndege za kijeshi kulenga ngome zao kitu kilichowafanya wajibu mashambulizi ili kujihami.

Kanali Kazarama amesema kumekuwa na mapigano makali katika Miji ya Kibati na Uvira lakini Jeshi la Serikali FARDC limeshindwa kuwadhibiti kutokana na wapioganaji wao kuwa imara kukabiliana na mashambulizi yaliyokuwa yanaelekezwa kwao.

Mapigano hayo yamezuka umbali wa kilometa nne kutoka Mji wa Goma ambao umekuwa ukisakwa kwa udi nauvumba na Wapiganaji wa Kundi la Waasi la M23 kitu kilichochangia maelfu ya wakazi kutoka Kibati kukimbilia mji huo kwa ajili ya kujiepusha na madhara ya vita hivyo.

Hakuna taarifa zozote zinazoeleza idadi ya majeruhi au vifo kutoka kwa Jeshi la Serikali FARDC wala Kundi la Waasi la M23 kutokana na mapigano hayo makali yaliyoshuhudiwa katika Miji ya Uvira na Kabati.

Mapema Serikali ya Kinshasa kupitia Msemaji wake na Waziri wa Habari Lambert Mende Omalanga alilinyoshea kidole cha lawama Kundi la Waasi la M23 kwa kutekeleza uhalifu katika Mji wa Kiwanja.

Mende amesema taarifa walizonazo zimeonesha Wapiganaji wa Kundi la M23 walivamia nyumba kumi pamoja na kuwapora wanafanyabiashara kumi na tano kabla ya kuua vijana kumi na watatu ma kisha wakabaka wanawake saba na kuwajeruhi wengine kumi na tatu.

Jeshi la Serikali la FARDC wamejiapiza kuendelea kuulinda Mji wa Goma kwa gharama yoyote ili kuwazuia Wapiganaji wa Kundi la Waasi la M23 kuutwaa Mji huo kama walivyofanya awali.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.