Ban Ki Moon na Koffi Annan wazuru Urusi na Uchina huku mapambano yakishuhudiwa jijini Damascus
Mapambano makali kati ya wanajeshi wa serikali na wapiganaji wa upinzani nchini Syria yameshuhudiwa mjini Damascus, mapigano yanayoelezwa na wanaharakati kuwa huenda yakaamua mustakabali wa machafuko nchini humo ambayo yamedumu kwa miezi 16 sasa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakati makabiliano yakiendelea, Urusi inasema itazuia mpango wowote wa mataifa ya Magharibi kupitisha azimio lolote dhidi ya serikali ya rais Bashar Al Assad.
Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov ameongeza kuwa Moscow haitaunga mkono kuongezewa muda kwa waangalizi wa kijeshi wa Umoja wa Mataifa waliokoo nchini Syria ikiwa uongozi wa rais Assad utaendelea kutishwa.
Morroco nayo imemtaka balozi wa Syria nchini mwake kuondoka Rabat kutokana na mauji yanayoendelea kushuhudiwa nchini Syria.
Huku Urusi ikiendelea kushikilia msimamo wake wa kuunga mkono uongozi wa rais Assad, msuluhishi wa kimataifa kuhusu mzozo huo Koffi Annan na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon wanazuru nchini Urusi na Uchina kujaribu kuwashawishi viongozi wa mataifa hayo mawili kubadilisha misimamo yao kuhusu mzozoro wa Syria.
Ziara hii inafanyika wakati baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa likiwa na siku nne kujadili na kuamua ikiwa waangalizi wa kijeshi wa Umoja huo wataendelea kuwa nchini Syria au la.
Mataifa ya Urusi na Uchina yameendelea kupinga kupitishwa kwa azimio lolote dhidi ya uongozi wa Damascus katika baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kwa kile mataifa hayo yanasema suluhu la Syria liko mikononi mwa wananchi wa Syria wenyewe.