Kiongozi wa msafara wa waangalizi wa UN nchini Syria ataka kusitishwa kwa mapigano kusaidia raia mjini Homs
Mkuu wa msafara wa waangalizi wa Umoja wa Mataifa walioko nchini Syria, Jenerali Robert Mood amezitaka pande mbili zinazopigana nchini humo kuruhusu wananchi walionaswa kwenye miji yenye mapambano kuondoka.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo amekiri kuwa mpango wao walioanza juma moja lililopita wa kutaka kuwahamisha maelfu ya wananchi toka mji wa Homs ambao umekuwa kwenye mapigano kwa muda mrefu umegonga mwamba kutokana na kukosa ruhusa kuingia mjini humo.
Mood ameongeza kuwa waangalizi wake wamekuwa kwenye hatari kubwa ya kushambuliwa na wanajeshi wa serikali ama wale wa upande wa jeshi huru la Syria pindi walipojaribu kuingia kwenye mji huo.
Jenerali Mood ametoa tangazo hilo saa chacahe baada ya kutangaza kusitisha operesheni zote za waangalizi wa Umoja wa Mataifa walioko nchini humo kufuatia hatari ya kushambuliwa ambapo amesema wataanza kazi hiyo pindi wakihakikishiwa usalama ama vinginevyo.
Jumuiya ya Kimataifa imeendelea kutaka kuchukuliwa kwa hatua za dharura dhidi ya machafuko yanyoendelea nchini Syria huku baadhi ya nchi zikitaka rais Bashar al-Asad kuondoka madarakani kupisha serikali ya muungano.
Kwa mujibu wa mashirika ya kutetea haki za binadamu nchini humo yanadai kuwa zaidi ya familia 1000 zimenaswa kwenye machafuko yanayoendelea kwenye mji wa Homs na kwamba wanahitaji msaada wa haraka kunusuriwa kwenye machafuko hayo.