Senegal: Kampeni za uchaguzi zinatamatika leo
Nairobi – Nchini Senegal, leo ndio siku ya mwisho ya kampeni kuelekea uchaguzi unaosubiriwa wa urais, utakaofanyika siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Wagombea 17 wamekuwa wakizunguka nchi hiyo ya Afrika Magharibi, kwa wiki mbili sasa kunadi sera zao kwa wapiga kura wapatao Milioni 7.3 watakaofanya uamuzi wao siku ya Jumapili.
Senegal inatarajiwa kuwa na rais mpya, baada ya kiongozi aliye madarakani Macky Sall kumaliza muhula wake wa pili, na kufikia Aprili 2 anatarajiwa kuondoka madarakani.
Hatimaye uchaguzi huu utafanyika baada ya hapo awali, kutokea kwa sintofahamu baada ya kuahirishwa mpaka mwezi Desemba lakini kutokana na shinikizo za ndani na nje, ikaamuliwa kuwa ufanyike Machi tarehe 24.
Wachambuzi wa siasa za Senegal, wanasema ni vigumu kufahamu ni nani ataibuka mshindi, na iwapo hilo litafanyika katika mzunguko wa kwanza, hata hivyo kufanyika kwa uchaguzi huo ni ahueni kwa raia wa nchi hiyo.
Hata hivyo, wagombea wawili wakuu ni Bassirou Diomaye Faye mwenye umri wa miaka 43, kutoka muungano wa kisiasa wa upinzani, anayeungwa mkono na mwanasiasa maarufu Ousmane Sonko, aliyezuiwa kuwania.
Mwingine ni Waziri Mkuu wa zamani Amadou Ba, mwenye umri wa miaka 62, anayeungwa mkono na rais anayeondoka madrakani Macky Sall.
Masuala muhimu kwenye kampeni hii inayomalizika ni kuhusu namna ya kuimarisha uchumi wa nchi hiyo na kupambana na ukosefu wa ajira hasa kwa vijana