Senegal: AU yatoa wito wa kufanyika mazungumzo katatua mzozo wa kisiasa
Nairobi – Mwenyekiti wa tume ya Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat, ametoa wito wa kusuluhishwa kwa mizozo ya kisiasa nchini Senegal kupitia njia ya mazungumzo na mashauriano.
Imechapishwa:
Wito wa AU umekuja baada ya kushuhudiwa makabiliano kufuatia hatua ya kuhairishwa kwa tarehe ya uchaguzi mkuu wa mwezi huu.
Faki aidha ametoa wito kwa mamlaka kuandaa uchaguzi huo haraka kama ilivyopangwa na kwa njia ya uwazi na haki
Rais wa Senegal Macky Sall alitangaza kuwa uchaguzi wa tarehe 25 ya mwezi Februari umehairishwa.
Wito wa AU unakuja wakati huu pia wabunge nchini humo wakitarajiwa pia kukutana kujadili hatua hiyo ya Sall ambayo imeibua mzozo kwenye taifa hilo.
Wabunge hao wanakutana siku moja baada ya kutokea kwa maandamano jijini Dakar, tukio ambalo lilipelekea kukamatwa kwa mwanasiasa wa upinzani.
Rais Sall katika taarifa yake ya Jumamosi ya wiki iliopita, alieleza kuwa amechukua hatua ya kusongesha mbele tarehe ya uchaguzi mkuu kwa sababu ya mzozo kati ya bunge la kitaifa na mahakama ya kikatiba kuhusiana na suala la baadhi ya wagombea kuzuiliwa kuwania.
Mahakama ya katiba ilimzuia Karim Wade, mwanawe rais wa zamani Abdoulaye Wade kutowania katika uchaguzi mkuu wa urais.
Wade alizuiliwa kwa madai ya kuwa na uraia wa nchi ya Ufaransa.