SADC: Mawaziri wa afya wakataa wito wa kutangaza dharura kuhusu kipindupindu
Nairobi – Mawaziri wa afya kutoka nchi za SADC, wametupilia mbali mapendekezo ya kutangaza dharura kuhusu msambao wa ugonjwa wa kipindupindu kwenye ukanda huo.
Imechapishwa:
Sylvia Masebo, Mwenyekiti wa kituo cha kudhibiti msambao wa magonjwa barani Afrika (CDC) katika taarifa yake hapo jana Jumatano, alisema ni jukumu la nchi binafasi kuamua iwapo itatangaza ugonjwa huo kama dharura ya la.
Akizungumza wakati wa kikao kisichokuwa cha kawaida cha CDC jijini Addis Ababa, Ethiopia, Masebo, ambaye pia ni waziri wa afya nchini Zambia, alitoa wito kwa nchi wanachama kuweka mikakati ya kuzuia msambao wa maambukizo hayo zaidi.
Aidha waziri huyo amethibitisha kwamba karibia nchi wanachama 15 wa Sadc zimeathiriwa na msambao wa kipindupindu.
Zambia ni miongoni mwa mataifa yanayokabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo ambao umetajwa kuwa mbaya zaidi katika kipindi cha miongo kadhaa.
Karibia watu 600 wamethibitishwa kufariki baada ya kuambukizwa wakati wengine zaidi ya elfu 16 wakiripotiwa kuambukizwa tangu mwezi Oktoba mwaka jana.
Zambia imeshuhudia mlipuko wa kipindupindu karibia mara 30 tangu mwaka wa 1977, maambukizo ya mwaka huu yakitajwa kuwa mabaya zaidi tangu mwaka wa 2017. Zimbabwe na Malawi nazo pia zimeathirika na ugonjwa huu.
Haya yanajiri wakati huu wakuu wa nchi za Sadc wakitarajiwa kufanya kikao kisichokuwa cha kawaidia kwa njia ya mtandao hapo kesho Ijumaa kuangazia namna mataifa wanachama yamejiandaa kukabiliana na ugonjwa huo kwenye ukanda wao.