Senegal: Mkutano wa upinzani kumteua mgombea urais umepigwa marafuku
Nairobi – Mamlaka nchini Senegal imepiga marufuku mkutano wa kumteua kiongozi wa upinzani anayetumikia kifungo jela Ousmane Sonko kugombea katika uchaguzi wa urais wa 2024, kwa mujibu wa afisa kwenye taifa hilo.
Imechapishwa:
Sonko mwenye umri wa miaka 49 amekuwa katikati ya mzozo na serikali ya taifa hilo ambao umedumu kwa zaidi ya miaka miwili na kuzua matukio kadhaa ya machafuko mabaya yaliotokona na maandamano ya wafuasi wake waliokuwa wanapinga kukamatwa kwa kiongozi wao.
Sonko alikuwa amewasilisha azma yake ya kugombea katika baraza la katiba ili kushiriki uchaguzi wa Februari licha ya serikali kukataa kumpa stakabadhi muhimu za kushiriki zoezi hilo.
Kwa mujibu wa barua iliyotiwa saini na gavana wa Dakar, Cherif Mouhamadou Blondin Ndiaye, mkutano wa Jumamosi ulipigwa marufuku kutokana na kile ambacho mamlaka imesema ni kumekuwepo na hofu ya kuvuruga utulivu wa umma, kuhitilifiana na usafirishaji huru wa watu na bidhaa.
El Malick Ndiaye, msemaji wa chama kilichofutwa cha Sonko Pastef, kupitia ukurasa wa facebook, alikashifu hatua hiyo ya serikali kuzuia mkutano huo.
Mamlaka ziliamuru Pastef avunjwe Julai.
Mgombea anayeunga mkono chama hicho Bassirou Diomaye Faye, ambaye pia yuko gerezani, pia amewasilisha stakabadhi za kugombea katika uchaguzi wa urais wa Februari.
Sonko aliondolewa katika sajili ya wapiga kura nchini Senegal baada ya kuhukumiwa mwezi Juni kifungo cha miaka miwili jela kwa tuhumza za kuwarubuni vijana.
Amekuwa jela tangu mwisho wa Julai kwa mashtaka mengine, ikiwa ni pamoja na kutoa wito wa uasi, kula njama na makundi ya kigaidi, na kuhatarisha usalama wa serikali.
Licha ya hayo, mwanasiasa huyo wa upinezani, amekana mashtaka hayo akisema yanalenga kumzuia kushiriki uchaguzi wa Februari 25.
Rais Macky Sall, ambaye alichaguliwa mnamo 2012 na kuchaguliwa tena mnamo 2019, mnamo Julai alitangaza kwamba hatawania muhula wa tatu. Alimchagua waziri mkuu wake, Amadou Ba, kama mgombea urais wa muungano wake.